Dar es Salaam. Huenda viongozi watano wa Chadema akiwemo mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe wakalala tena katika gereza la Segerea kutokana na utaratibu za kuwalipia faini ya zaidi ya Sh100 milioni kutokamilika hadi leo Jumatano Februari 12, 2020 saa 8:30 mchana.
"Hadi sasa hatujafanikiwa kupata removing order itakayowezesha kuwatoa viongozi wengine waliobakia katika gereza la Segerea. Hatuna uhakika kama leo hii watatoka. Tutatoa taarifa hapo baadaye,” amesema John Mrema, Mkurugenzi wa Itikadi, uhusiano na mambo ya nje wa Chadema katika mkutano na waandishi wa habari leo Jumatano Machi 12, 2020.
Viongozi wanane wa Chadema pamoja na aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Vicent Mashinji Jumanne Machi 10, 2020 walihukumiwa kulipa faini ya Sh350 milioni au kwenda jela miezi mitano baada ya kutiwa hatiani kwa makosa 12 kati ya 13 yaliyokuwa yanawakabili.
Washtakiwa hao wakiongozwa na Mbowe walilazimika kwenda jela baada ya kushindwa kukamilisha taratibu za kulipa faini hiyo waliyohukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Baada ya hukumu hiyo iliyosomwa na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, Chadema walianza kuchangishana fedha kwa ajili ya kuwalipia faini viongozi wake hao.
Jana Chadema walifanikisha kuwalipia faini ya Sh110 milioni wabunge Esther Matiko (Tarime Mjini), Ester Bulaya (Bunda) na Halima Mdee (Kawe) ambao wametoka jela leo asubuhi.
Habari zinazohusiana na hii
- Chadema wasema bado Sh90 milioni kuwatoa jela viongozi wote
- MPYA: Hakimu amaliza kupitia uchambuzi wa mashahidi kesi ya kina Mbowe - VIDEO
- VIDEO: Rais Magufuli amlipia Mchungaji Msigwa faini ya Sh38 milioni
- VIDEO: Mdee, Bulaya na Matiko watoka jela
Ambao bado wapo katika gereza la Segerea ni Mbowe, John Heche (Tarime Vijijini), John Mnyika (Kibamba), naibu katibu mkuu wa chama hicho-Zanzibar, Salum Mwalimu na Mchungaji Peter Msigwa ambaye leo amelipiwa Sh38 milioni na Rais John Magufuli.
Endelea kufuatilia Mwananchi kwa taarifa zaidi