Dodoma. Mbunge wa Kigoma Kusini (CCM), Husna Mwilima amemtaka Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina kumwondoa mmoja wa watumishi wa wizara hiyo mkoani Kigoma, aliyemtaja kwa jina moja la Judith.
Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi mwaka 2019/2020, leo Jumanne Mei 21, 2019, Mwilima amesema mtumishi huyo amepelekwa Kigoma wakati wabunge wa kanda ya ziwa wamemkataa.
“Kila mwezi anaripoti Takukuru kwa madudu aliyofanya, anakuja Kigoma ziwa Tanganyika kuua uvuvi. Wewe Waziri ni msikivu tafuta mahali pengine pa kumpeleka Kigoma hatumtaki.” Amesema mbunge huyo.
Amesema mtumishi huyo amepelekwa kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria, lakini anaharibu utaratibu wa ziwa.
“Kuna mtu anaitwa Francis Kabure, huyu ni Mrundi, ameshaomba uraia mara tatu amenyimwa anapewa cheo cha kuwa mwenyekiti wa wavuvi wakati hakuchaguliwa bali amechaguliwa na Judith,” amesema.
Amehoji ana maslahi gani na mtu huyo na kutaka waondolewe mtu huyo kwa sababu hana sifa ya kuendelea kuwa msimamizi.