Dodoma. Mbunge wa Ukerewe (CCM) Joseph Mkundi amemtaka Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina kutoa tamko la kuachilia mashine za wavuvi ambazo wanazishikilia.
Mkundi ameyasema hayo leo Jumatano Mei 22 2019 wakati akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi mwaka 2019/2020.
Amesema operesheni dhidi ya uvuvi zimekuwa na madhara kwa wavuvi na kwamba yeye amekuwa muumini wa kulinda rasilimali lakini hakubaliani na madhara yanayosababishwa na operesheni hizo.
“Huyu mwanamama Judy (aliyetajwa na Mbunge wa Kigoma Kusini Husna Mwilima CCM) amewasababishia madhara mengi wavuvi. Wamenyanyaswa wamenyang’anywa nyavu zao lakini mbadala wake nini baada ya kuwanyang’anya?” Amehoji.
Amesema kuwa asilimia 90 ya vijana wanajihusisha na uvuvi na kwamba dhahiri unapogusa unaathiri kundi hilo.
Ametaka ufafanuzi kuhusu nyavu zinazotakiwa katika kuvua dagaa. “Samaki aina ngere, furu, ningu wanavuliwa kwa utaratibu upi? Kwa sheria ipi? Serikali itoe tamko ni vipi samaki hao watavuliwa ,”amesema Mkundi.
Pia Soma
- UCHOKOZI WA EDO: Hili la korosho, kuna umuhimu wa kuchutama yaishe
- Meno ya tembo yapeleka wanne jela miaka 20 kila mmoja
- Shahidi aeleza bosi wake alivyoongozana na gari lenye shehena ya dhahabu
Amesema kupungua kwa aina hiyo ya samaki hakutokani na kuvuliwa bali ni kwa sababu wanaliwa na samaki aina ya sangara.
“Mashine hadi leo zimeshikiliwa, wapewe waendelee na shughuli zao. Serikali ilinde rasilimali lakini tuimarishe watu wetu tunapochoma moto tutoe na mbadala,”amesema.
Mwisho