Dodoma. Mbunge wa Iramba Mashariki (CCM), Alan Kiula ameitaka Serikali kutowapa miradi Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa maelezo kuwa wana miradi mingi hawajaikamilisha.
Kiula ameeleza hayo leo Jumatano Januari 29, 2020 bungeni mjini Dodoma katika mjadala wa taarifa za kamati za Bunge za Hesabu za Serikali (PAC) na Serikali za Mitaa (Laac) zilizowasilishwa bungeni.
Mbunge huyo amesema haiwezekani TBA kuendelea kulundikiwa miradi mkubwa wakati hawana uwezo wa kujenga hata miradi midogo jambo alilodai linasababisha miradi mingi kutokamilika.
Amesema kamati yao ilizunguka maeneo mengi na kushuhudia utendaji wa kusuasua pamoja na uchunguzi uliofanywa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
"TBA wasipewe mradi wowote hapa nchini hadi wamalize viporo walivyonavyo vinginevyo hali haitakuwa nzuri kwa miradi mingi waliyonayo," amesema Kiula.