MBUNGE wa jimbo la Sengerema Hamis Mwagawa'Tabasamu' ameiomba Serikali iwasaidie katika ukamilishaji wa miradi ya maji katika wilaya yao.
Akizungumza wakati wa kikao cha kwanza cha bodi ya barabara ya mkoa wa Mwanza kwa mwaka wa fedha 2020/2021,Tabasamu alisema miradi ya Maji bado ina ubabaishaji mwingi sana.
‘’Nimezungumza na mkaguzi wa Hesabu za serikali(CAG) tukague hii miradi inatesa sana wananchi kwasababu pesa nyingi zimetumika na miradi haijakamilika’’ alisema Tabasamu
Alisema Mradi wa maji wa Buyagu umeanza mwaka 2014 na umegharimu bilioni 1.7/-,mradi wa Katunguru ulianza mwaka 2019 na umegharimu milioni 730 na miradi hiyo yote haijakamilika.
Tabasamu alisema mradi wa maji Nyamazugo umegharimu bilioni 23/- na mpaka sasa haujakamilika takribani kwa miaka mitatu.
Alisema mradi wa Nyampande haujakamilika na umetumia bilioni 1.35/-.
Katika utekelezaji wa maendeleo ya miradi ya barabara, Mwagawa alisema kuna changa moto ya utekelezaji katika wakala wa barabara (Tanroad) katika utoaji wa taarifa za miundo mbinu.
Alisema anaiomba Tanroad wawe wanatoa ramani za barabara ili wananchi waweze kujua ni aina gani za barabara zinazojengwa katika maeneo yao.