Dodoma. Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF), Maftaha Nachuma amehoji iwapo Rais John Magufuli amemteua Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga ili awafukuze viongozi wa chama chake.
Akiomba mwongozo wa Spika bungeni leo, Maftaha alisema mkuu huyo wa wilaya amekua na tabia ya kuwafukuza wenyeviti wa CUF na kwamba jana alimfukuza mwenyekiti mwingine.
“Leo wakati nakuja bungeni nimepata simu ikieleza kuwa mkuu wa wilaya ya Chemba anaendeleza kuwafukuza viongozi wa CUF, suala hili limenifanya nishindwe kufanyakazi zangu vizuri,” alisema na kuongeza:
“Mwenyekiti naomba mwongozo wako, Rais amemteua mkuu huyu wa wilaya kuwafukuza viongozi wa CUF tu na si viongozi wa vyama vingine?”
Akijibu mwongozo huo, Mwenyekiti wa Bunge, Najma Giga alisema Serikali imesikia na kwamba itafanyia uchunguzi suala hilo.