Dodoma. Mbunge wa Malindi (CUF) Ally Saleh amesema Zanzibar haikushirikishwa katika uandaaji wa Muswada wa Sheria ya Kutangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi wa Mwaka 2018.
Akizungumza katika mjadala wa muswada huo bungeni leo Jumanne Septemba 4, 2018, Saleh amesema kumekuwa na utaratibu wa kutowashirikisha Zanzibar katika sheria zinazohusu Muungano na ndio maana zimekuwa zikikataliwa na Baraza la Wawakilishi.
"Mfano Sheria ya deep sea ( bahari kuu) ilipitishwa kimabavu hapa ikaenda kule Baraza la Wawakilishi ikakataliwa," amesema.
Hata hivyo, Spika wa Bunge Job Ndugai mara baada ya mbunge huyo kumaliza kuzungumza, alimjibu kuwa waliopo bungeni ni wawakilishi wa wananchi wa pande zote mbili za Muungano.