MBUNGE wa Makete kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Festo Sanga, ameiomba serikali kuligeukiwa shamba la maaalum la kitulo la Ng'ombe wa maziwa ambao wana uwezo wa kuzalisha lita 40 hadi 50 kwa siku.
Sanga ameyasema hayo leo katika ziara yake kwenye shamba hilo ambalo lilianzishwa na Hayati Mwalimu Julius Nyerere kwa lengo la viwanda vya Tanzania kuzalisha maziwa yatokanayo na ng’ombe wa hapa nchini.
“Shamba hili ni la muda mrefu, ndio shamba pekee Afrika Mashariki lenye ng'ombe wanaotoa lita 40 hadi 50 kwa siku, lakini kwa muda mrefu limekuwa halikui na ng'ombe hawaongezeki.” alisema
Aidha Sanga amemuomba Rais John Magufuli na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kuchukua hatua za makusudi kuhakikisha shamba hilo linakuwa na tija hasa ikiwa ni kuzalisha maziwa ya kutosha kwa watanzania wote.
Alisema kwa sasa shamba hilo halina vifaa vya kisasa vya kuendeshea shughuli za shamba, lakini majengo ni chakavu, na idadi ya mifugo imekuwa ikipungua badala ya kuongezeka.