Chama cha Mapinduzi (CCM) kimesema kimepokea kwa masikitiko barua ya kujiuzulu kwa Mbunge Mteule wa CCM Jimbo la Konde Sheha Mpeka Faki leo August 02, 2021
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Agosti 2 na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, Faki ameandika barua ya kujiuzulu ambapo ameeleza kufikia uamuzi huo kutokana na changamoto za kifamilia.
Shaka amesema chama hakina uwezo wa kumzuia katika uamuzi wake huo hasa ikizingatiwa ni haki yake ya msingi kama ilivyo kwa haki ya kuomba ridhaa ya kugombea nafasi ndani ya CCM na kuwaomba wanachama wote kuwa watulivu katika kipindi hiki wakati wakisubiri taratibu nyingine.
Amejiuzulu kabla hajaapishwa na Spika wa Bunge zikiwa zimepita siku 14 tu tangu alipochaguliwa katika uchaguzi uliohusisha pia chama cha ACT-Wazalendo ambacho kilipoteza jimbo hilo.
Faki alichaguliwa katika uchaguzi mdogo uliofanyika Julai 18 ambapo CCM ilishinda katika jimbo hilo pamoja na kata sita zilizoshiriki uchaguzi huo ambapo ilishinda bila kupingwa katika kata nne miongoni mwa hizo.