Dodoma. Mbunge wa Ndanda (Chadema), Cecil Mwambe amemuomba Rais John Magufuli kuagiza kuchunguzwa kwa kampuni ya Sicpa inayoendesha mradi wa stempu za kodi za kielektroniki (ETS) kwa madai kuwa inaiibia nchi.
Sicpa inaendesha mradi huo kwa kuweka stempu za kielektroniki katika eneo ambalo bidhaa zinazalishwa.
Akizungumza jana Jumatatu Juni 17, 2019 katika mjadala wa bajeti kuu ya Serikali mwaka 2019/2020 bungeni jijini Dodoma Mwambe alisema, “Naomba nitoe kielelezo cha pili kinachoonyesha ubadhirifu mkubwa ikiwa ni pamoja na taarifa za PPRA (Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma) katika gazeti (la kila siku) wakionya namna Sicpa ilivyopata tenda ya kutengeneza stempu.”
“Kama Rais Magufuli anasikia tunavyosema hapa hatua ya kwanza kuchukua ni kuichunguza kampuni hii ya kisanii ambayo Uganda na Kenya walikataa kufanya nayo kazi.”
Mwambe alisema, “Wanachokifanya wao ni kuhesabu, mfano pakiti moja ya sigara ni Sh8 lakini Serikali inapata Sh3. Tunataka kufahamu kwa nini mtu anayefanya kazi ya kuhesabu anapata fedha nyingi tofauti na Serikali inavyokusanya katika eneo hilo.”
Mwambe alisema gharama za stempu ni kubwa kuliko gharama za kodi zinazokusanywa na Serikali, kutaka majibu ya Serikali kuhusu tenda iliyopewa kampuni hiyo na mkataba husika ukoje.
Pia Soma
- Wanawake washikana ‘uchawi’ kwenye chaguzi
- Rais Magufuli amtengua Mwenyekiti Bodi ya REA
- Bunge la EALA kujadili bajeti ya 2019/20 ya Sh249.8 bilioni