Dodoma. Mbunge wa Mchinga (CUF), Hamidu Bobali amesema atajiuzulu ubunge ikiwa mbunge au waziri atathibitisha kuwa wakulima wa korosho hawalipwi Sh2,640 badala ya Sh 3,300 kwa kilo moja kama ilivyoahidiwa na Rais John Magufuli.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Februari 2, 2019 bungeni jijini Dodoma katika mjadala wa taarifa za kamati za Bunge za Bajeti na Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC).
Bobali amesema Rais Magufuli alitangaza kuwa wakulima wa korosho watalipwa Sh3,300 kwa kila kilo moja ya korosho.
Amesema badala yake wakulima wamekuwa wakilipwa Sh2,640 kwa kilo moja ya korosho wakati hakuna tamko la kubadilisha bei ya awali.
Kauli hiyo ya Bobali ilimnyanyua naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Stella Manyanya na kubainisha kuwa mbunge huyo amelidanganya Bunge.
Kauli hiyo ya Manyanya ilizua hali ya sintofahamu bungeni baada ya wabunge kubainisha kuwa kanuni aliyotumia Manyanya kusimama na kupinga maelezo ya Bobali haipo katika kanuni za Bunge.
Alipopewa nafasi ya kuendelea na mchango wake, Bobali alirudia kauli yake hiyo.
“Kama kuna mbunge ama waziri anapinga hili na kudhibitisha kuwa mimi nasema uongo najiuzulu ubunge. Rais alisema wakulima watalipwa moja kwa moja Sh3,300 ni tamko gani imebadilisha bei hiyo,” amehoji Bobali.