Dodoma. Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Dk Jasimin Tisekwa ameishauri Serikali ya Tanzania kuangalia upya utaratibu wa urejeshaji wa mikopo ya elimu ya juu kwa sababu badala ya kumsaidia mtoto wa masikini umekuwa ni mzigo.
Akichangia katika mapendekezo ya bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 ya Sh33.1 trilioni, leo Ijumaa Juni 21 2019 amesema pamoja na uzuri wa mikopo hiyo lakini kuna changamoto zake.
“Mkopo huu pamoja na uzuri wake lakini kuna changamoto ambazo badala ya kumsaidia mtoto wa masikini vinakuwa mzigo,” amesema.
Dk Tisekwa amesema mfano wa kijana aliyemaliza chuo mwaka 2015 anapewa msamaha wa miaka miwili kabla ya kuanza kulipia mkopo huo kwa utaratibu wa makato ya asilimia 15.
Ametoa mfano wa mwanafunzi aliyemaliza chuo mwaka 2015, alianza kulipa baada ya miaka miwili ambaye alichukua mkopo wa Sh10 milioni lakini hivi sasa anadaiwa Sh 16.5 milioni.
“Mikopo imekuwa kama ni biashara kwa kweli itaathiri sekta ya chuo kikuu kama Serikali ilivyochukua hatua za haraka kurekebisha kama kwenye kodi ya pad (taulo za kike) kwa kuondoa kodi,” amesema.
Pia Soma
- Wingu zito mhandisi aliyejinyonga Chunya
- Maandalizi ya maonyesho ya sabasaba yaanza
- Ujenzi meli mpya Ziwa Vitoria wafikia pazuri
“Kozi za sayansi zinazochukua muda mrefu zitaathirika kwa sababu ya huu utaratibu wa Value Retention Fund ni mzigo umeongezwa kwa watoto wa masikini,”amesema Dk Tisekwa.
Amesema mkopo huo umekuwa haumaliziki hadi mtu anapozeeka na kwamba bila kuangalia inaweza kuwa kichocheo cha rushwa.
Aidha, ameishauri Serikali kutoa fedha za ujenzi za hosteli katika vyuo ili kuepusha madhara yanayoweza kuwapata wanafunzi.