Dodoma. Mbunge wa Bunda (CCM), Mwita Getere amemuomba Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai kuruhusu wabunge kukatwa posho ya siku moja ili fedha zitakazopatikana wapewe mawaziri wachapa kazi huku akimtaja aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola.
Getere ameeleza hayo bungeni mjini Dodoma leo Jumatano Februari 5, 2020 katika mjadala wa taarifa ya kamati ya Bunge ya Nishati na Madini.
Huku akiwataja mawaziri wanne kwa maelezo kuwa ndio wachapakazi, mbunge huyo amesema, “hata huyu pacha wangu Lugola amechapa kazi nzuri sana anastahili pongezi, lakini hiyo ajali aliyopata itapita ila amefanya mema.”
Amesema mawaziri hao wachapakazi ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dk Hussein Mwinyi; Waziri wa Madini, Dotto Biteko na Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani huku akisema Dk Mwinyi amevuka vikwazo na ameshinda vishawishi vyote.
Akimchambua Biteko, amesema ni kijana mzuri anayetakiwa kuandaliwa vema ili kwani miaka ya baadaye atakuwa kiongozi mzuri na kwamba Dk Kalemani anazunguka sana na kumaliza kero za umeme kwenye maeneo yaliyoshindikana.
Uteuzi wa Lugola ulitenguliwa na Rais John Magufuli baada ya kiongozi mkuu huyo wa nchi kumtaja Lugola kuhusika katika mkataba wenye utata ambao kampuni moja ya Romania iliingia na wizara hiyo.