Dodoma. Mbunge wa Nanyamba (CCM) Abdallah Chikota amesema hali ya uzalishaji wa mazao ya biashara nchini Tanzania si nzuri na kuishauri Serikali kuwekeza katika kilimo kama ilivyowekeza kwenye mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR).
Chikota alikuwa akichangia mapendekezo ya bajeti ya Serikali ya mwaka 2019/2020 ya Sh33.1 trilioni bungeni leo Alhamisi Juni 20, 2019.
Amesema suala la kuongeza muda wa msamaha kwa walipa kodi kutoka miezi mitatu hadi mitano ni jambo zuri sana.
“Nawapongeza Serikali kwa dhati kabisa kwa kuanza kufanya maboresho ya mfumo wa udhibiti wa biashara na kuondoa tozo 54,”amesema.
Hata hivyo, amesema kilimo ni eneo ambalo linatoa mchango kwenye pato la Taifa na Watanzania wengi wameajiriwa lakini mazao ya biashara uzalishaji wake umeporomoka sana na kwamba hilo sio nzuri.
“Changamoto kubwa ni kwamba hatujawekeza vya kutosha. Nishauri Serikali yangu tutoe macho kwenye sekta ya kilimo kama tulivyowekeza sasa hivi katika Standard Gauge (SGR),”amesema.
Pia Soma
- Mkenya kortin kwa kusafirisha madini ya Sh500 milioni
- Mfanyabiashara kortin kwa kusafirisha dhahabu kinyume cha sheria
- Aliyehukumiwa miaka 20 kwa kubaka, akabiliwa na kesi mbili za kubaka
“Tutoe mikopo rafiki kwa wakulima maalum kwa riba nafuu pamoja na upatikanaji wa mbegu na pembejeo za uhakika. Tuwekeze katika ubanguaji wa Korosho kwa kuhamasisha viwanda vipya,” amesema.
Amesema Msumbuji wana taasisi maalum ambayo inaangalia Korosho katika ubanguaji, pembejeo na soko la Korosho.
Mbunge huyo amesema Tanzania inatakiwa kujifunze kutoka kwa Msumbiji.