Dar es Salaam. Mbunge wa Kibaha Vijijini (CCM) Hamoud Jumaa amewasihi viongozi wa dini kuwaombea ili wachaguliwe tena katika uchaguzi ujao na ikiwezekana wapite bila kupingwa.
Alisema hayo jana Jumatano, Juni 5, 2019 katika maadhimisho ya Baraza la Eid El Fitr lililofanyika jijini Tanga ambako Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alikuwa mgeni rasmi.
Baada ya salamu viongozi kutolewa na ulipowadia wa Jumaa alianza kwa kusema kila aliyesimama kutoa salamu alikumbusha kuwaombea viongozi wa juu pekee huku wabunge wakisahaulika katika maombi hayo.
“Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba kawataja Rais na waziri mkuu waombewe dua, kaja Naibu Waziri wa Maji, Jumaa Aweso kamtaja Rais na waziri mkuu pia. Sijajua waziri mkuu atasema nini, pamoja na Mufti ila na mimi naomba niongeze tu, Mufti tuombee na sisi wabunge vilevile tuchaguliwe tena na ikiwezekana tupite bila kupingwa maana uchaguzi umekaribia,” amesema
Mufti wa Tanzania, Abubakar Zubeir alimtoa hofu mbunge huyo na kuahidi kuwaombea huku akimtaka aamini watarudi katika nafasi zao kwa sababu wao ndiyo wako karibu na wananchi.
“Najua sasa hivi wako katika sintofahamu ya nitarudi au sitarudi, ‘Insha-Allah’ Mwenyezi Mungu atawajaalia mtarudi, na masheikh muwaombee hawa ndiyo tunashirikiana nao katika mengi. Hata Mtume aliposema mtu akiwafanyia wema mlipeni sisi hatuwezi, ila tutawaombea hivyo niwaombe ndugu zangu wa taasisi mbalimbali tuwaombee viongozi wetu kwa kuanza na Rais, waziri mkuu, mawaziri, wabunge na viongozi wengine,” amesema Mufti Zubeir.