Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ametoka katika gereza la Segerea leo jioni Ijumaa Machi 13, 2020 baada ya kukamilisha kulipa faini ya Sh70 milioni.
Mbowe ambaye ni mbunge wa Hai alihukumiwa kulipa faini hiyo baada ya kutiwa hatiani katika mashtaka nane yakiwemo ya uchochezi.
Leo saa 6: 15 mchana Mwananchi limeshuhudia mmoja wa wanachama wa Chadema akitoka kugongewa mhuri na mhasibu wa mahakamani ya Hakimu Mkazi Kisutu baada kutoka benki kulipa kiasi hicho cha fedha.
Baada ya kukamilisha taratibu zote, mwanachama huyo amelieleza Mwananchi kuwa wanaelekea Segerea kwa ajili ya kumtoa Mbowe.
Akizungumza na Mwananchi mkurugenzi wa itikadi, uhusiano na mambo ya nje wa Chadema, John Mrema amesema, “Mbowe ametoka jioni hii na hivi sasa anakuja katika ofisi za makao makuu ya chama akiwa na watu wengine.”
Mbowe ni kati ya viongozi wanane wa Chadema ambao pamoja na aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Vicent Mashinji Jumanne Machi 10, 2020 walihukumiwa kulipa faini ya Sh350 milioni au kwenda jela miezi mitano baada ya kutiwa hatiani kwa makosa 12 kati ya 13 yaliyokuwa yanawakabili.
Habari zinazohusiana na hii
- Mbowe alipa faini, muda wowote kutoka jela
- Wanachama wa Chadema watawanywa kwa mabomu ya machozi gereza la Segerea
- VIDEO: Mchungaji Msigwa azungumzia uhusiano wake na Rais Magufuli
- VIDEO: Msigwa afunguka kuhusu kilichotokea gerezani, asema aliwaachia vumbi
Baada ya hukumu hiyo iliyosomwa na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, Chadema walianza kuchangisha fedha kwa ajili ya kuwalipia faini viongozi wake hao.
Hadi leo saa 6:00 mchana viongozi wa Chadema waliotoka jela ni katibu mkuu wa chama hicho, John Mnyika; naibu katibu mkuu-Zanzibar, Salum Mwalimu; mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko.
Wengine ni mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche; mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa; mbunge wa Kawe, Halima Mdee na Ester Bulaya (Bunda). Mbowe pekee ndiye alikuwa amebaki jela.
Dk Mashinji alitoka Jumatano baada ya kulipwa faini ya Sh30 milioni na CCM. Mchakato wa kumlipia faini Dk Mashinji uliongozwa na katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Humphrey Polepole.
Hata hivyo, Mdee; Bulaya; Meya wa Ubungo, Boniface Jacob; katibu wa chama hicho Mkoa wa Dar es Salaam, Henry Kileo na mjumbe wa baraza la Vijana Chadema (Bavicha), Hadija Mwago wamekamatwa leo walipofika katika gereza la Segerea kufuatilia taratibu za kumtoa Mbowe.
kwa sasa wanaelekea gereza la Segerea kwa ajili ya kumtoa Mbowe.
Hukumu hiyo, iliyolewa Machi 10, 2020 na hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Thomas Simba.
Mpaka sasa viongozi wote wa chama hicho, wameshalipiwa faini.