Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mbowe: Vyama vimekufa kwa kuzuiwa kufanya mikutano ya hadhara

97567 Pic+mbowe+3 Mbowe: Vyama vimekufa kwa kuzuiwa kufanya mikutano ya hadhara

Mon, 2 Mar 2020 Chanzo: mwananchi.co.tz

Hai. Mbunge wa Hai (Chadema), Freeman Mbowe amesema kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara kumeviathiri vyama vingi vya upinzani na kwamba baadhi vimekufa.

Mbowe ambaye pia ni mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ametoa kauli hiyo jana Jumamosi Februari 29, 2020  wakati  akihutubia kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Snow View, Bomang'ombe.

Amesema nchi ilishapiga hatua katika ujenzi wa demokrasia ya vyama vingi, lakini sasa  imerudi nyuma miaka 20.

"Miaka minne na nusu hatujawahi kufanya mikutano ya kisiasa na tukifanya mizengwe kibao  matokeo ya kuzuiwa kwa mikutano hii ni kwamba kuna vyama zaidi ya 20 vya siasa nchini, lakini vingine ni kama vimekufa na kama kipo ni Chadema na kidogo ACT-Wazalendo,” amesema  Mbowe.

"Vyama vingine vingi vimekufa  kwa sababu haviwezi kufanya mikutano tunakwenda wapi. Vyama vya siasa vimeruhusiwa kikatiba na sheria na ili visikike ni lazima vizungumze na wananchi.”

"Akija Chadema anazungumza kwa uhuru wake, akija CCM azungumze kwa uhuru wake na akija ACT Wazalendo na vyama vingine kila kimoja azungumze kwa uhuru wake. Rais (John Magufuli) alipoingia madarakani  akazuia mikutano yote ya vyama vya siasa, jambo ambalo ni kinyume kabisa na sheria na polisi wakishaambiwa ni amri,” amesema Mbowe.

Habari zinazohusiana na hii

Advertisement
Amebainisha kuwa hakuna kiongozi aliye juu ya sheria na ili nchi iweze kuwa na utawala bora wenye kuheshimiana ni lazima wote kwa pamoja kuheshimu sheria za nchi.

"Tulijenga mageuzi kwa miaka 25 lakini kuna mambo yanapindishwa halafu mnategemea viongozi tusiseme, tutasema hadi siku tunaingia kaburini, acha wanasiasa wakaseme, wananchi waamue, na kama serikali yako ni safi kwa nini unaogopa?” amehoji Mbowe.

 

Kompyuta yake yaibiwa

Juzi  watu wasiojulikana wamevamia nyumbani kwa katibu wa Mbowe, Irene Lema na kuiba Ipad na kompyuta mpakato yenye nyaraka mbalimbali za mbunge huyo wa Hai.

Walivamia wakati Irene akiwa katika mkutano wa Mbowe uliofanyika  jana katika viwanja vya Nkoromu kata ya Masama kati wilayani Hai.

Imedaiwa kuwa kompyuta hiyo ina kumbukumbu za ofisi pamoja na siri za Mbowe.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Salum Hamdun alithibitisha kutokea kwa tukio hilo, na kueleza kuwa katibu huyo alimlalamikia juu ya tukio hilo  alipofika katika kituo cha polisi Bomang’ombe, muda mfupi baada ya Mbowe kukamatwa na polisi.

 

 

Chanzo: mwananchi.co.tz