Dodoma. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ametangaza chama hicho kikuu cha upinzani nchini Tanzania kufuta mikutano yake iliyopangwa kuanza kufanyika Arpili 4, 2020 ili kuepuka kuenea kwa maambukizi ya ugonjwa wa corona.
Kiongozi huyo ameishauri Serikali ya Tanzania kuzuia mikusanyiko isiyokuwa ya lazima ikiwemo ibada na katika masoko na kwamba watu wapewe utaratibu wa kupata mahitaji yao muhimu.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Machi 23, 2020 mjini Dodoma, Mbowe amesema wamefanya hivyo kuunga mkono juhudi za Serikali kukabiliana na ugonjwa huo uliosababisha vifo vya watu zaidi ya 13, 000 duniani kote.
Amebainisha kuwa ratiba ya mikutano hiyo itatolewa baadaye hali itakaporejea kama awali.
Amesema chama hicho hakiingilii uhuru wa watu kuabudu lakini ni njia mojawapo ya kukabiliana na ugonjwa huo aliodai kuwa kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) unaua watu kati ya 800 hadi 1,000 kwa siku.
"Hatutaki siasa kwenye mapambano dhidi ya corona kila mwananchi achukue hatua ya kujilinda na ugonjwa huu hatari na ikibidi Serikali itoe elimu ya kutosha kwa wananchi namna ya kujilinda.”
Habari zinazohusiana na hii
- Chadema kuanza mikutano ya hadhara Tanzania nzima kuanzia Aprili 4
- VIDEO: Chadema kuendelea na maandalizi ya mikutano ya hadhara