Dar es Salaam. Madiwani watano wa Chama cha ACT-Wazalendo manispaa ya Kigoma Ujiji leo Jumatano Februari 12, 2020 wamejiuzulu na kujiunga na CCM.
Wametangaza uamuzi huo katika ofisi ndogo za CCM zilizopo mtaa wa Lumumba, jijini Dar es Salaam . mbele ya katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally na katibu wa itikadi na uenezi wa chama hicho tawala nchini Tanzania, Humphrey Polepole.
Madiwani hao ni Hamis Rashid (Gungu), Abduli Nasoro (Kasingirima), Foard Sefu (Kasimbu), Ismael Husen (Kagera) na Mussa Ngongolwa (Kipampa).
Akizungumzia kuhama kwa madiwani hao, Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mawasiliano na Umma wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu amesema, “sisi msimamo wetu watu wanapotoka ACT kwenda vyama vingine tunawatakiwa kila la kheri kwani inakuwa ni uamuzi binafsi.”
“Kulikuwa na jitihada za muda mrefu za kuwashawishi madiwani wa Kigoma Ujiji kujiunga na CCM na kinachotokea sasa ni matunda ya ushawishi mkubwa ukihusisha ahadi mbalimbali na madiwani hawa wameshindwa kuhimili vishawishi hivyo.”
Ameongeza, “bado tunaongoza Halmashauri na tutaendelea kuiongoza, Meya na Naibu Meya ni wa ACT-Wazalendo na bado hatutayumba kwenye uchaguzi mkuu kwani madiwani hao hawatoi taswira ya wananchi wa Kigoma ambao bado wanatuamini.”