Arusha. Siku tano baada ya kujiuzulu na kuhamia CCM, waliokuwa madiwani wa Chadema katika Jiji la Arusha wameeleza sababu ya kuchukua uamuzi huo.
Wakizungumza leo Jumatano Januari 29, 2020 baada ya kupokewa na mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Arusha Mjini, Joseph Masawe wametaja sababu hizo.
Aliyekuwa diwani wa Olorieni, Zakaria Mollel amesema amejiunga CCM ili kushirikiana na Rais John Magufuli kufanya kazi za maendeleo katika kata yake.
“Wanaofikiri nimekuja CCM kwa kuhongwa waongo maana mimi ni mfanyabiashara hakuna wa kunihonga na Chadema nilitumia fedha zangu kukijenga chama hicho,” amesema Mollel.
Aliyekuwa diwani wa Themi, Melace Kinabo amesema ametoka Chadema kwa sababu ya kupata vikwazo vya maendeleo.
"Chadema kuna siasa za kutotenda naamini nimekuja huku (CCM) baada ya kuomba kanisani, kwamba nikaungane na Rais Magufuli kuleta maendeleo ya kasi,” amesema.
Pia Soma
- Kobe Bryant kupewa tuzo ya Oscar
- Bruno Fernandes atua Manchester United kwa vipimo vya afya
- Yanga yazigomea adhabu za Bodi ya Ligi, yashtaki CAF
Akizungumza baada ya kuwapokea wanachama hao wapya, Massawe amesema wamekwenda CCM wakati muafaka, “kikubwa cha kufanya ni kufuata taratibu za chama na tunawakaribisha sana.”
Katibu wa CCM Wilaya ya Arusha, Denis Zakaria amesema chama chao hakijafunga milango kwa wanachama wapya.