Mwanga. Baraza la Halmashauri ya wilaya ya Mwanga, limeahirishwa kwa dakika 30 kumpa nafasi ofisa utumishi wa halmashauri hiyo, Steven Ubavu kuwasilisha ushahidi wa barua za kuwarudisha watumishi waliohamishwa kwa utata kama alivyoagiza na Waziri mkuu, Kassim Majaliwa.
Hayo yametokea leo Ijumaa Februari 6, 2020 baada ya wajumbe wa baraza hilo kutilia mashaka majibu ya ofisa utumishi huyo ambaye ni kaimu mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, kwamba barua hizo zimeandikwa na mkurugenzi wa Halmashauri, Zefrin Lubuva ambaye hakuwepo katika kikao hicho.
Diwani wa Kigonigoni, Jeremiah Shayo alieleza kuwa Majaliwa alitoa agizo kuwa watumishi walioandikiwa barua za onyo zifutwe na waliohamishwa kurejeshwa kwenye vituo vyao vya awali lakini hakuna kilichofanyika.
"Mwanga hatuna mhandisi hata mmoja wameondoka kwa sababu wanaona CV zao zinachafuliwa kwa kuandikiwa barua za onyo. Sisi kama wajumbe wa kamati ya fedha hatuko tayari kuona Halmashauri inateteleka," alisema diwani huyo.
Baada ya hoja hiyo, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Theresia Msuya alimtaka ofisa huyo kutoa maelezo na kujibu kuwa maagizo yote yaliyotolewa na viongozi wa juu yametekelezwa.
Madiwani wengi hawakuridhika na majibu hayo na mwenyekiti kuagiza kikao kusimama kwa dakika 30 ili kamati ikae na kumuagiza ofisa huyo kuleta barua za uthibitisho.