Morogoro. Baraza la Madiwani Manispaa ya Morogoro limekataa ombi la wenyeviti wa Serikali za mitaa 294 kuwatenga posho ya Sh10,000 kwa mwezi kutokana na ufinyu wa bajeti unaoikabili manispaa hiyo.
Akizungumza wakati wa kuwasilisha mapendekezo ya bajeti ya mwaka 2020/2021 katika mkutano maalumu wa Baraza la Madiwani la halmashauri hiyo, Ofisa Utumishi wa halmashauri hiyo, Waziri Kombo amesema kwa sasa hawana ubavu wa kuwapatia posho ya mwezi ya Sh10,000 wenyeviti wa Serikali za mitaa.
Kombo ameyasema hayo wakati akijibu hoja ya Diwani wa Kata ya Kuchangani, Gilbert Mtafani aliyependekeza wenyeviti hao wapatiwe posho hiyo kwa mwezi ili kuwaepusha na vishawishi vya rushwa wakati wa kutoa huduma kwa wananchi.
“Halmashauri yetu haiwezi kuwapatia posho ya Sh10,000 kwa mwezi wenyeviti 294 wa Serikali za mitaa kutokana na mapato yanayokusanywa kuwa madogo, pengine katika siku zijazo huenda katika bajeti zijazo zinaweza, lakini siyo kwa sasa, hatuwezi kutokana na ufinyu wa mapato kidogo ya ndani,” amesema Kombo.
Kombo amesema kuwa halmashauri ambazo zinaweza kuwalipa posho wenyeviti hao ni zile zinazokusanya mapato ya ndani kiasi cha Sh50milioni au Sh60 milioni kwa mwezi ambazo zinaweza kuwalipa hata Sh25,000 kwa mwezi.
Katika hoja yake, diwani huyo amesema kuwa wenyeviti hao wamekuwa wakifanya kazi nyingi na hivyo umefikia wakati wa kutengewa bajeti ili kuwaondoa na kutowaingiza katika tuhuma za rushwa pindi wanapowahudumia wananchi.
Pia Soma
- Simulizi ya mwanafunzi aliyepona corona
- Aliu: Familia ya watoto watano wanaotamba katika udaktari
- Nida yakwama usajili wa namba, vitambulisho