Chifu Mkuu Kanda ya Kati Dodoma, Henry Mtemi wa pili Mazengo amesema suala la Mbunge wa kuteuliwa, Humphrey Polepole kusema Machifu si kitu chochote wanaleta ukabila halina mashiko na linapaswa kukemewa.
Chifu Mazengo alisema hayo jana jijini hapa wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema machifu wana umoja ndio maana serikali inatambua na kuthamini mchango wao.
Aidha, Chifu Mazengo alisema ni muhimu kwa Watanzania wote kuungana kwa pamoja kulinda amani ya Tanzania si kuleta mkanganyiko katika jamii.
Kuhusu suala la kumtafuta Mbunge Polepole, Chifu Mazengo alisema amefanya kila namna hakupata ushirikiano na kuona suluhu pekee ni kukimbilia kwenye vyombo vya habari.
Katika hatua nyingine, Chifu Mazengo ameshauri viongozi mbalimbali kuwa mstari wa mbele kufuata maadili kwani wao ndio waongoza njia.
Chifu Mazengo pia amewahimiza Watanzania kujitokeza zoezi la sensa ya watu na makazi ili kuweza kuhesabiwa kwa maendeleo ya nchi pamoja na kuhamasisha kuchanjwa chanjo ya Covid-19.
Februari 2, mwaka huu, Polepole alinukuliwa akisema: “Mambo ya Machifu hayana msaada kwa Taifa, yanaweza kuleta ukabila na mgawanyiko, yanapaswa kupingwa.”