Dar es Salaam. Saa chache baada ya Mahakama Kuu kutengua uteuzi wa wajumbe wa bodi ya wadhamini wa Chama cha Wananchi (CUF), Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad ameitaka ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kufanya ukaguzi wa fedha za ruzuku za chama hicho.
Maalim Seif alitoa kauli hiyo leo Jumatatu Februari 18, 2019 wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za wabunge wa chama hicho, Magomeni jijini Dar es Salaam.
Amesema baada ya uamuzi huo wa mahakama ni vyema CAG, akafanya ukaguzi kwa kuwa bodi hiyo iliyokuwa kambi ya mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba haikuwa halali.
"Tumeupokea kwa furaha uamuzi huu wa Mahakama Kuu, umekata mzizi wa fitina wa madai yetu dhidi ya Rita. Nilishasema toka awali tutapokea uamuzi wowote wa mahakama utakaotolewa,” amesema Maalim Seif.
"Nawaomba wanachama wa CUF wawe watulivu kwa sasa wakati tukisubiri uamuzi mwingine utakaotolewa hapo Ijumaa," amesema Maalim Seif.