Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Maagizo ya CCM kwa wakandarasi wabovu

968a36d57d7d0def1e90c4de75d0906a Maagizo ya CCM kwa wakandarasi wabovu

Mon, 20 Sep 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) wilaya ya Geita mkoani Geita, Barnabas Mapande ametoa wito kwa viongozi wa Halmashauri ya Mji wa Geita kuhakikisha wanafuatilia mienendo ya wahandisi wa serikali ambao ni wazembe kusimamia miradi ya umma.

Mapande ametoa wito huo juzi alipotembelea mradi wa ujenzi wa shule ya mpya ya msingi ya Kijiji cha Samina Kata ya Mtakuja katika mwendelezo wa ziara ya kamati ya siasa ya wilaya kukagua utekelezaji wa ilani ya CCM kwa mwaka 2021.

Mapande alisema imekuwepo shida ya baadhi ya wahandisi wa halmashauri kutofanya ukaguzi na ufuatiliaji wa miradi ya kijamii na kusababisha wakandarasi kutokamilisha miradi ya ujenzi kwa wakati na ujenzi kutekelezwa chini ya kiwango hivyo wahandisi wa aina hiyo wanapaswa kuwajibishwa.

“Tunachelewa kwa sababu ya hawa wakaguzi ambao kimsingi wanapaswa wakague ili ujenzi uendelee na wananchi wamlipe fundi, watalaamu hawatoi maelekezo, wananchi wanajiendea tu, ndio maana utakuta kuna kasoro kwenye majengo mengi.

“Wahandisi wetu wanalalamikiwa, tunawaomba waje kukagua miradi tuendelee na ujenzi hawaji, tunachelewa kwa sababu yao, nikuombe Mkuu wa Wilaya, uwasiliane na viongozi wetu wa halmashauri waone kwa nini wahandisi wetu wanachelewa kukagua miradi,”alisema.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Geita, Wilson Shimo ameahidi kufanyia kazi maelekezo hayo huku akiwaagiza maofisa ardhi kushirikiana na viongozi wa mitaa kuhakikisha maeneo yote inapojengwa shule na zahanati yawe yamepimwa kuepusha taharuki yoyote.

Awali akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa shule, Ofisa Elimu Kata ya Mtakuja, Deusdedith Nchamba alisema mradi umetumia fedha za uwajibikaji wa kampuni kwa jamii (CSR) Sh milioni 100, mchango wa mbunge matofali 2,000, mchango wa diwani mifuko ya saruji 50, nguvu ya wananchi sawa na Sh milioni 15.

Chanzo: www.habarileo.co.tz