Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Lowassa atamani tena ubunge wa Monduli

17417 LOWASA+PIC TanzaniaWeb

Sun, 16 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Arusha. Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa amesema anatamani angekuwa na uwezo wa kugombea tena ubunge katika Jimbo la Monduli ili kusimamia na kupinga vitendo vya uvunjaji wa Katiba ya nchi.

Kwa mujibu wa Lowassa ambaye alishawahi kuongoza jimbo hilo kwa miaka 20, kuna mambo yanaendelea nchini ambavyo havimfurahishi.

“Ndugu zangu wana Monduli, mambo yanayoendelea kwa sasa, hasa nchi hii yanahitaji Katiba mpya, tena itakayotoa adhabu kwa yoyote atakayekiuka au kwenda kinyume, ikiwamo haya ya kuwanyima wapinzani kugombea, kuongoza au kufanya siasa kwa kuwatisha, kuwateka na kuwalaghai,” alisema Lowassa.

“Yaani natamani ningeweza nigombee tena, mngeona kama ningeruhusu haya, ila kwa sababu siwezi, basi naombeni mpeni kura Yonas Laizer maana nitakuwa nampa mbinu za kufanya na msikubali kuibiwa siku hiyo, mkiletewa fujo wamama naombeni pigeni ukunga wa mwizi nasi tutawasaidia,” aliongeza.

Awali, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema baada ya chaguzi hizi za marudio kupita, Chadema watakuwa na ajenda kuu ya kudai haki zinazovunjwa wakati ziko kwenye Katiba.

Mbowe alisema kuwa kuzuia matangazo ya moja kwa moja ya Bunge, kuzuia mikutano ya siasa na viongozi wa vyama vya siasa kutishwa ni uvunjaji mkubwa wa Katiba, hivyo wanavuta kasi kuanzisha ajenda mpya ya kudai kufuatwa kwa Katiba

“Rais anapoingia madarakani mbali na kuapa na kitabu cha dini yake, pia anaapa kulinda, kupigania na kutetea Katiba ya nchi,” alisisitiza.

Alisema jambo kubwa linalowaumiza wapinzani, mbali na kukatazwa kufanya mikutano ya hadhara ya kuwashukuru wananchi kwa kuwachagua, hata wale waliochaguliwa katika uchaguzi uliopita wanatishwa, kutekwa na wale warahisi wanalaghaiwa kwa fedha na madaraka.

“Tufikie hatua wananchi tujue hakuna mtu aliye juu ya sheria , si kiongozi wala mtawala bali haki na wajibu vifuatwe ikiwamo wananchi kugombea na kuchaguliwa bila kujali wanawakilisha chama gani,” alisema.

Mbowe alieleza kushangazwa na wagombea wa CCM kutumia viongozi wa Serikali kuwapigia kampeni kwa magari ya Serikali.

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema aliwataka wananchi wa Monduli kumchagua Laizer ili aweze kufichua maovu ya aliyekuwa mbunge Julius Kalanga ambaye kwa sasa anagombea kupitia CCM.

Laizer aliwataka wananchi wa Monduli wamchague ili ahakikishe anarudisha maji yaliyokuwa yanatiririka kila kijiji kwa jitihada za Lowassa, lakini kutokana na uzembe wa Kalanga alilimbikiza madeni hadi Sh100 milioni za umeme yaliyosabishwa maji kukatwa.

“Nichagueni jamani nihakikishe namuumbua Kalanga juu ya wananchi wa Monduli ardhi ya Monduli kukosa ardhi na wengine wasio wakazi wakaipata,” alisema Laizer.

Chanzo: mwananchi.co.tz