Dar es Salaam. Chama cha Wananchi (CUF) nchini Tanzania kinatarajia kuanza ziara katika mikoa mbalimbali nchini kwa lengo la kuhamasisha uchaguzi wa serikali za mitaa na uandikishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.
Mkurugenzi wa Habari na Mahusiano ya Umma wa CUF, Abdul Kambaya amesema hayo leo Jumatatu Septemba 30, 2019 wakati akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya chama hicho Buguruni jijini Dar es Salaam.
Amesema ziara hiyo itaambatana na viongozi wakuu watatu wa chama hicho wakiongozwa na Mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Lipumba.
Kambaya amesema Profesa Lipumba atafanya ziara hiyo inayoanza kesho Jumanne Oktoba 1, 2019 katika mikoa ya Tabora, Simiyu, Shinyanga, Mwanza, Mara, Geita, Kagera na Kigoma.
Amesema Makamu Mwenyekiti wa CUF-Bara, Naftah Nachuma atakuwa katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma wakati Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho- Bara, Magdalena Sakaya ataelekea Morogoro, Singida na Manyara.
"Pamoja na mambo yote, ziara hii itafanya tathmini ya uchumi na maisha ya Watanzania," amesema kiongozi huyo wa idara ya habari na mawasiliano ya umma.
Pia Soma
- Mfalme Saudia Arabia: Nawajibika kwa kifo cha mwandishi Kashoggi
- Lugola aagiza askari wote kituo cha polisi wahamishwe
- Dk Bana: Kutoka mwalimu chekechea, mhadhiri wa Udsm mpaka kuwa balozi - VIDEO
Amesema watakachofanya ni kutoa taarifa kwa makamanda wa polisi wa wilaya husika kama sheria inavyowataka.