Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kuelekea Tanzania ya Demokrasia, wadau watakiwa kujitokeza

Bende Mchakato unahusu ruhusa ya mikutano ya hadhara

Sat, 16 Apr 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wadau wakaribishwa kutoa maoni,nyaraka na michango mbalimbali itakayotumika kufanya maboresho katika maeneo tisa yaliyobainishwa na Kikosi Kazi kilichokuwa kikipitia na kuchambua maoni yaliyotokana na mkutano wa wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa nchini uliofanyika tarehe 15, 16 na 17 Desemba 2021 jijini Dodoma.

Hayo yamebainishwa na Katibu wa Kikosi Kazi hicho Sisty Nyahoza kupita taarifa kwa umma iliyotolewa ambapo wadau wanaarifiwa kuanza kwa mchakato wa kupokea na kuwasilisha maoni yao kwa kikosi kazi hicho ndani ya siku 31 tangu kutolewa kwa taarifa hii.

Wito huo umekuja ikiwa ni baada ya Kikosi kazi hicho kilichoanza kazi rasmi tarehe 11 Januari 2022 ya kupitia na kuchambua maoni na mapendekezo yote yaliyotolewa na washiriki wa mkutano wa wadau na baadaye kikaainisha maeneo tisa mahususi ya kufanyia kazi kwa ustawi wa demokrasia nchini.

“Ili Kikosi Kazi kiweze kutekeleza kazi zake kwa mujibu wa mpango Kazi uliopo, mnaombwa kuwasilisha maoni, mapendekezo au nyaraka hizo, ndani ya muda wa siku thelathini na moja (31) kuanzia tarehe ya leo 14 Aprili 2022.” Ilisisitiza sehemu ya taarifa hiyo.

Taarifa hiyo imeyabainisha maeneo hayo kuwa ni pamaoja na; mikutano ya hadhara na ndani ya vyama vya siasa, masuala yanayohusu uchaguzi, mfumo wa maridhiano ili kudumisha haki, amani, utulivu na Umoja wa kitaifa.

Maeneo mengine ni ushiriki wa wanawake na makundi maalumu katika siasa na demokrasia ya vyama vingi vya siasa, Elimu ya Uraia, Rushwa na Maadili katika Siasa na Uchaguzi, Ruzuku ya Serikali kwa Vyama vya Siasa, Uhusiano wa Siasa na Mawasiliano kwa Umma pamoja na Katiba Mpya.

“Hivyo, Kikosi Kazi kinaalika taasisi, kikundi cha watu na mtu yeyote mwenye maoni, mapendekezo au nyaraka kuhusu masuala hayo tisa au mengine yoyote yanayohusu demokrasia ya vyama vingi vya siasa, ambayo anaona yatasaidia Kikosi Kazi kuandaa mapendekezo mazuri na yanayotekelezeka, awasilishe maoni, mapendekezo au nyaraka hizo,” ilisema taarifa hiyo.

Taarifa hiyo imeainisha njia za kuwasilisha maoni hayo kuwa ni pamoja na Barua pepe, [email protected], ujumbe WhatsApp kwenda kwa Katibu wa Kikosi Kazi kupitia namba 0784 394883, Sanduku la Posta, 2851 Dodoma;

Njia nyingine iliyoainishwa ni kuwasilisha moja kwa moja katika Ofisi za Msajili wa Vyama vya Siasa zilizopo; Dodoma viwanja vya Nanenane Nzuguni, katika Jengo la Wizara ya Kazi, Mtaa wa Nzuguni A; Dar-es Salaam, mtaa wa Shaaban Robert mkabala na Shule ya Msingi Bunge na Zanzibar, mtaa wa Mbweni Matrekta.

Aidha kupitia taarifa hiyo kikosi kazi kimebainisha kuwa pamoja na kukusanya na kupokea maoni kwa njia tajwa hapo juu kinaandaa utaratibu maalumu utakaotumika kukaribisha taasisi, vikundi na watu maalum kuzungumza nao, iii kupata ufafanuzi wa maoni na mapendekezo yao.

Kikosi Kazi hiki kimetokana na Mkutano wa wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa uliofanyika tarehe 15, 16 na 17 Desemba 2021 Dodoma, ambapo ulifunguliwa na Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kufungwa na Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

Baada ya mkutano huo washiriki walipendekeza na Serikali ikaridhia kwamba, kiundwe Kikosi Kazi ambacho kitachambua maoni na mapendekezo yaliyojitokeza na kuandaa mapendekezo mahususi ambayo yatawasilishwa Serikalini kwa ajili ya kufanyiwa kazi.

Tarehe 23 Desemba 2021 Kikosi Kazi hicho kiliundwa na kilizinduliwa tarehe 10 Januari 2022 na Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Kikosi Kazi kilianza kazi tarehe 11 Januari 2022 ambapo bado kinaendelea na kazi hiyo kama kilivyoelekezwa wakati wakiwasilisha taarifa ya awali mbele ya Rais Samia Suluhu Hassan mapema hivi karibu.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live