Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kubenea ahoji sababu umeme kukatika Dar

59442 KUBENEAPIC

Fri, 24 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dodoma. Mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea amesema bado kuna shida ya umeme jijini Dar es Salaam kutokana na kukatika mara kwa mara huku akiitaka Serikali kutoa majibu ya jambo hilo.

Kubenea ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Mei 24, 2019 bungeni jijini Dodoma wakati akiuliza swali la nyongeza huku akiyataja  maeneo ya Kigamboni, Ukonga, Ubungo na Kibamba kuwa na tatizo hilo la kukatika kwa umeme licha ya mradi wa kuzalisha umeme wa Kinyerezi kuwa katika maeneo hayo.

Akijibu swali hilo la nyongeza, naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amesema hali ya kukatika kwa umeme si kubwa kama ilivyokuwa mwanzo.

Kuhusu kutoa taarifa ya kukatika kwa umeme, Mgalu amesema huwa zinatolewa kupitia makundi ya mtandao wa kijamii wa WhatsApp yaliyoundwa katika kila kandana kwamba hata yeye yupo katika kundi la wadau wa umeme eneo la Kibamba.

Katika swali la msingi, mbunge wa Kibamba (Chadema), John Mnyika amehoji ni kwa nini jimbo la Kibamba umeme unakatika mara kwa mara huku akishangazwa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kutopunguza gharama za kuunganisha umeme kwa wateja wake waliopo maeneo ya mbali.

Akijibu swali hiyo Mgalu amesema kukatika umeme Kibamba  kunatokana na kuhamisha miundombinu ya umeme ili kupisha upanuzi wa barabara ya Morogoro -Dar es Salaam.

Pia Soma

Kuhusu gharama za kuunganishiwa umeme, amesema zimepungua katika maeneo ya pembezoni mwa majiji na kuhusu gharama wanazotumia kuunganisha  kutoka mbali, amesema kuna sheria ya majadiliano kati ya shirika na mteja.

Chanzo: mwananchi.co.tz