Dar es Salaam. Makatibu wakuu wa zamani wa CCM, Abdulrahman Kinana na Yusuf Makamba leo Jumatatu Februari 10, 2020 wameitikia wito wa kamati ya maadili ya chama hicho tawala nchini Tanzania iliyowaita kwa ajili ya kuwahoji.
Leo mchana walifika katika ofisi ndogo za chama hicho zilizopo mtaa wa Lumumba, Dar es Salaam na kupokelewa na makamu mwenyekiti wa chama hicho, Philip Mangula pamoja na katibu mkuu, Dk Bashiru Ally.
Kufika kwao huenda kukamaliza mjadala wa kinachoendelea juu yao baada ya taarifa ambazo hakuna upande uliozithibitisha iwapo wamejiuzulu uanachama wa CCM na kupoteza sifa za kuhojiwa.
Taarifa za Kinana na Makamba kujiuzulu zilisambaa mitandaoni na Mwananchi lilidokezwa kuwa barua zao za uamuzi huo wameziwasilisha ofisi ya katibu mkuu wa CCM zikiambatanishwa na kadi zao za uanachama.
Baada ya kuwasili baadaye Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Humphrey Polepole alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akielezea kufika kwao.
“Wamefika kuitikia wito wa kamati ndogo ya usalama na maadili inayoongozwa na ndugu Mangula. Kinana na Makamba wamefika katika ofisi hizo mchana na kupokelewa na Mangula na Dk Bashiru,” amesema Polepole katika taarifa hiyo.
Habari zinazohusiana na hii
- Wanahabari wasota ofisi za CCM Dodoma kumsubiri Kinana
- SINTOFAHAMU: Kinana, Makamba giza nene
- UDHIBITI WA MAKADA NDANI YA CCM: Maelezo ya Membe yaacha maswali
- Kinana, Makamba sasa shubiri CCM
Membe alifika mbele ya kamati hiyo yenye wajumbe wanne Alhamisi iliyopita Februari 5, 2020 makao makuu ya CCM Dodoma, alihojiwa kwa zaidi ya saa 5 na baadaye akawaeleza waandishi wa habari jinsi alivyofurahishwa na mahojiano hayo na kuwa Mungu alimpa ujasiri wa kuzungumza kile alichotaka kuiambia kamati hiyo na hakuyum-ba wala kuyumbishwa.