Morogoro. Kesi ya jinai inayowakabili wabunge wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na wenzao watano imeendelea kuahirishwa hadi Machi 18, 2020 baada ya upande wa Jamhuri kukabiliwa na changamoto ya kupeleka mashahidi mahakamani.
Wabunge hao ni Peter Lijualikali (Kilombero) na Susan Kiwanga wa Mlimba.
Akizungumza kabla ya kesi hiyo kuahirishwa leo Jumatatu Februari 24, 2020, Wakili wa Serikali, Calistus Kapinga amesema Jamhuri inakabiliwa na changamoto ya kupeleka mahakamani mashahidi kutokana na mashahidi kuwa nje ya Morogoro.
Kapinga amesema kuwa Machi 18, 2020 Jamhuri itajitahidi kupeleka mashahidi ili kesi hiyo iweze kuendelea kusikilizwa.
Kwa upande wa wakili wa washtakiwa, Hekima Mwasipu, akisaidiana na Jonathan Mndeme wamesema shauri hilo lilikuwa chini ya Hakimu, Elizabeth Nyembele ambaye kwa sasa amehama Morogoro na mara ya mwisho liliahirishwa Desemba 2019.
Kabla ya kuahirisha kesi hiyo, Hakimu mkazi mfawidhi katika mahakama ya hakimu mkazi Morogoro, Abeesiza Kalegeya aliwasomea washtakiwa kifungu cha 214 (1) sheria ya mwenendo wa kesi ya jinai sura ya 20 kama ilivyorekebishwa 2002.
Pia Soma
- Bomu lajeruhi 29 mkutano wa Waziri Mkuu Ethiopia
- Makonda amtaka mratibu Tarura kuweka kambi Tamisemi
- Anayedaiwa kumuua mkewe kwa kumchoma moto ahoji jalada kuchapishwa miezi mitano
- Kabendera awashukuru waandishi wa habari, aanza kuomboleza kifo cha mama yake
Wabunge hao na wenzao wanashtakiwa mahakamani hapo kwa kesi ya jinai namba 43 ya mwaka 2019 na kwamba Novemba 26, 2017 walitenda makosa nane likiwamo la kuharibu mali na kuchoma moto ofisi ya Serikali ya kijiji cha Sofi Wilaya ya Malinyi wakati wa uchaguzi wa marudio wa udiwani.