Katibu wa CCM wa Mkoa wa Kilimanjaro, Jonathan Mabihya amesema migogoro pamoja na uhusiano mbaya wa viongozi kwenye chama hicho unakidhoofisha na kupunguza heshima kwa jamii inayowazunguka.
Amesema maeneo ambayo Serikali na chama hicho hakina uhusiano mzuri, matokeo yake ni kukwama kwa shughuli za maendeleo pamoja na wananchi kukosa huduma stahiki.
Mabihya ameyasema hayo jana Novemba 11, wakati wa semina ya viongozi wa ngazi za vitongoji, vijiji wa chama hicho katika jimbo la Same Magharibi iliyolenga kuwakumbusha watendaji hao uelewa wa majukumu yao ya kazi pamoja na kujenga umoja miongoni mwao.
"Nendeni mkawe na mahusiano mazuri yana faida kwenu, kwa chama na serikali na hali hiyo italeta matokeo chanya kwa wananchi pamoja na maendeleo kwenye maeneo yetu, wananchi hawapendi kuona uhusiano yetu yakiwa mbaya.
"Wananchi wanapenda na kuona ilani ya chama inatekelezwa, wanahitaji kuona shule, zahanati, barabara na mambo mengine mengi vinakuwepo kwenye maeneo yao na hili inawezekana endapo kuna mahusiano mazuri," amesema Mabihya.