Katika taarifa yao ya kuhitimisha ziara ya siku mbili mkoani Rukwa, wajumbe hao wakiongozwa na Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo, wamesema katika kusimamia utekelezaji wa ilani ya CCM ya 2020-2021, hawatamvumilia kiongozi au mtendaji serikalini atakayekuwa kikwazo katika kuitekeleza kwa ufanisi.
Wajumbe wengine ni Kanali mstaafu Ngemela Lubinga, ambaye ni Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Shaka Hamdu Shaka, Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi na Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Kenani Kihongosi.
Katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga, mkoani humo juzi, Chongolo alisema, ziara yao iliyoanza Julai 7 hadi 8 kutembelea mashina ya CCM, wameshuhudia miradi ambayo thamani ya fedha hailingani na viwango husika.
Chongolo alitoa mfano kwamba hospitali za wilaya za Nkasi na Kalambo, kila moja imepatiwa Sh. bilioni 2.3, lakini ujenzi hauridhishi kwa sababu thamini ya fedha hailingani na kazi iliyofanyika.
Kutokana na hali hiyo ya ovyo, Katibu Mkuu Chongolo alimwagiza Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Mkirikiti, kuhakikisha ndani ya siku zisizozidi 14 ujenzi wa hospitali hizo unalingana na thamani ya fedha na kwamba maelekezo hayo si porojo.
“Tunamaanisha, si kurembaremba, ni lazima tufanye kazi yenye tija,” alisema Chongolo katika kikao hicho kilichohudhuriwa na viongozi na watendaji wa CCM, viongozi na watendaji wa serikali, madiwani pamoja na wabunge.
“Wananchi wakiona mambo hayaendi, watatuona sisi tunapiga porojo na sisi hatuko tayari kuitwa wapiga porojo,” alionya.
Kero nyingine ambayo wananchi wanakumbana nayo ni ukosefu wa dawa katika hospitali, vituo vya afya na zahanati, licha ya serikali kutoa fedha nyingi kuwezesha wananchi kupata huduma hiyo.
Katibu Mkuu atawasiliana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Dk. Doroth Gwajima, pamoja na uongozi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD), kujua mamilioni ya fedha yanayotolewa kwa ajili ya kuwezesha upatikanaji wa dawa yanakwama wapi.
“Tunataka watueleze nani anasababisha mkwamo katika upatikanaji wa dawa. Nasema hivi, sisi viongozi tunawajibu wa kufuatilia na kusimamia thamani ya fedha katika kila eneo,” alisema.
Chongolo alisema kila kiongozi na mtendaji katika chama na serikali anawajibu wa kutimiza wajibu wake kwa kuhakikisha upatikanaji wa tija unakuwapo.
Kuhusu migogoro ya ardhi, Chongolo alimwagiza Mkirikiti pamoja na wakuu wa wilaya za mkoa wa Rukwa kutafuta suluhisho la kero hiyo, ambayo imekuwa ikipoteza muda mwingi wa wananchi, ambao wangeutumia katika uzalishaji mali.
Kwa upande wa maji alisema bado ni changamoto, na kudokeza kwamba ni wakati muafaka kuanza kufikiria kuwa na mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Tanganyika kwa ajili ya Mkoa wa Rukwa.