Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema hivi karibuni itatangazwa kamati maalumu itakayoshughulikia suala la upatikanaji wa katiba mpya ya Tanzania
Rais Samia alitoa kauli hiyo leo wakati wa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani yaliyoandaliwa na baraza la wanawake la Chadema (BAWACHA) ambapo amesema hakuna mtu anayekataa mchakato huo kuendelea
Aidha Kiongozi huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM amesema ilikuwa kazi ngumu kushawishi chama chake kukubali kurejeshwa kwa mikutano ya hadhara nchini huku akisema anafahamu pia ugumu alioupata mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe kumualika katika mkutano wa BAWACHA leo
Akizungumza katika mkutano huo Mwenyekiti wa CHADEMA freeman Mbowe amemtaka Rais wa Tanzania kuliangazia suala la wabunge 19 wa Chama hicho ambao wamefukuzwa na chama hicho huku akisema hawawakilishi chama wala wananchi bungeni
Kuhusu Katiba Mpya Mbowe amesema kuwa pamoja na mchakato wa katiba mpya kuendelea lakini kasi inahitajika zaidi ili kukamilisha mchakato huo kabla ya uchaguzi ujao.
Awali akizungumza katika mkutano huo Mwenyekiti wa BAWACHA taifa Sharifa Suleiman ameitaka serikali kuangazia suala la gharama za maisha kupanda ikiwa ni pamoja na kodi za umeme, maji, mlolongo wa kodi za biashara, mazingira magumu ya kibiashara, kilimo na mishahara duni.