Monduli. Mgombea wa Ubunge wa CCM, jimbo la Monduli, Julius Kalanga amemtaka Waziri Mkuu wa mstaafu, Edward Lowassa aache kumdhalilisha.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa soko la Mto wa Mbu, jana Agosti 31 Kalanga amesema amesikitishwa na kauli za Lowassa za kumdhamlilisha na kutoa maneno ya uongo hadharani.
Katika mkutano huo viongozi na wanachama wa Chadema zaidi ya 50, walitangaza kujiunga na CCM.
"Nimewaambia wazee wa kimila waone huyu mzee jinsi ambavyo hanitendei haki kwa sababu tu mimi ni masikini, anasema uongo kuwa nimejiuzulu ubunge baada ya kushindwa kulipa deni la milioni 600,"alisema.
Kalanga alisema ni kweli alikuwa Mbunge akiwa masikini, lakini Lowassa anajua kuwa nyumba yake (Kalanga) iliyopo Monduli haitoshi hata kuwekwa dhamana ya Sh100 milioni.
“Leo mzee niliyekuwa namuheshimu sana, kama baba yangu, ananichafua kuwa nimeondoka Chadema eti nimeshindwa kulipa deni na pia kasema mimi si riziki ...Nimetafakari sana maneno ya Baba yangu, yule lakini nimemuachia Mungu,"alisema.
Kalanga alisema wengi wamekasirishwa na kauli za Lowassa za kumdhalilisha na hivyo vijana zaidi ya 100 wa Mto wa Mbu wameamua kuhama chadema na kujiunga na CCM.
"Anasema nimekisaliti Chadema, ni kweli na nitaendelea kukisaliti kwa maslahi mapana ya wananchi wa Monduli,"alisema.
Kalanga alisema Lowassa anadanganya kuwa Monduli, haina shida ya maji, wakati wafugaji wa Monduli hawalali wakitafuta maji na akarejea kauli ya Mwalimu Julius Nyerere kuwa hatuwezi kuyakwepa matatizo kwa kutoyasema.
"Mimi nasema Monduli tuna shida ya maji na tunaomba serikali isaidie, Monduli bado tuna shida ya barabara serikali isaidie,"alisema.
Viongozi, wanachama Chadema wajiunga na CCM
Katika mkutano huo, viongozi na wanachama wa Chadema zaidi ya 50, akiwamo Mwenyekiti wa Baraza la vijana la Chadema wilaya ya Monduli, Yasini Shabani walitangaza kujiunga na CCM.