Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Jinsi Mbunge CUF alivyobadili gia angani

27900 MBUNGE+PIC TanzaniaWeb

Tue, 20 Nov 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Nani anahama na nani anabaki, lilikuwa swali lililogonga vichwa vya wengi Alhamisi iliyopita ya Novemba 15 ambayo kwa mujibu wa CCM, ilikuwa siku ya mwisho kwa wabunge na madiwani kutoka upinzani kupokelewa ndani ya chama hicho na kupewa nafasi ya kugombea tena.

Joto lilipanda na kuwavuruga wabunge hasa baada ya mbunge wa Temeke (CUF), Abdallah Mtolea kutangaza ndani ya Bunge kuwa anajiuzulu ubunge na kuomba chama kinachotaka kufanya kazi na yeye kujitokeza.

Kuondoka kwa Mtolea ambaye jioni ya siku hiyo alihamia CCM na kufanya idadi ya wabunge wa upinzani waliojiunga na chama hicho kufikia 10 inaweza kuwa haikushtua sana, badala yake Mbunge wa Tandahimba (CUF), Katani Katani ndiye aliyetawala mjadala bungeni na hasa kwenye mitandao ya kijamii.

Duru za siasa, zilidai kwa vile Katani alionekana katika viunga vya Bunge asubuhi akiwa na Mtolea, jambo hilo liliwahusisha wawili hao kujiuzulu na baadaye ikatajwa kuwa wabunge wawili, James Mbatia (Vunjo-NCCR-Mageuzi) na Selemani Bungara ‘Bwege’ (CUF) walimnasua Katani.

“Ni kweli Katani alikuwa miongoni mwa waliotakiwa kuhama siku hiyo (Alhamisi), lakini kuna wabunge wawili walizungumza naye sana na kumsihi asihame, alikuwa njiani kuhama kama alivyofanya Mtolea bungeni,” alisema mbunge mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Katani alipozungumza na Mwananchi alisema hana wazo la kuhamia CCM, “Na kama nikihama chama, siwezi kwenda CCM, hao walioandika kwamba naondoka walikuwa na hoja zao.”

Alipoulizwa taarifa za yeye kuwa karibu na Mtolea siku aliyotangaza kuhama, alisema, “Mimi na Mtolea ni zaidi ya marafiki, anapajua nyumbani, familia yangu, watoto na wazazi wangu, lakini hadi anaondoka sikuwa najua kitu.”

Katani akijibu swali kuhusu madai kuwa Mbatia na Bungara walichangia asihame siku hiyo alikanusha akidai hakuwa na mpango wa kuhama.

“Siyo kweli, wabunge wengi hawapafahamu kwangu na mimi siku hiyo nilipotoka bungeni nilikwenda nyumbani peke yangu na niliporudi nilimpitia Bwege tukaenda sote bungeni.”

“Mimi nina mtaji wa wananchi, niliwahi kuwaeleza wananchi wangu kuwa nikihama sitakwenda CCM, hata kama nikifukuzwa na (Profesa Ibrahim) Lipumba siwezi kwenda CCM,” alisema.

Alipoulizwa kama wanawasiliana na Mtolea tangu ahame, alisema; “Nawasiliana kwa simu, sijawahi kukutana naye, nikikutana naye na hali hii, wanaweza kusema vingine lakini mimi siwezi kuhama.”

Lakini, Bungara alisema alikuwa anahisi hilo kwa Katani baada ya Mtolea kuhama.

“Lakini Katani wakati wote alinieleza kwamba mimi (Katani) sina hizo na jioni nitakwenda kutoa kauli bungeni,” alisema.

Alipoulizwa mazungumzo hayo yalifanyikia wapi, Bungara alisema; “Tulikwenda kuyafanyia nyumbani kwake kuanzia saa 7 hadi 10 jioni tuliporudi bungeni.”

Alisema walipofika bungeni kabla ya kuingia ukumbini, waliwakuta wabunge wa Chadema wakizungumzia suala hilo la Katani kujiuzulu, na wao walipomuuliza Katani aliwajibu anakwenda kutoa kauli bungeni hivyo wakamsindikiza.

Mbatia ambaye imeelezwa alihusika kumshawishi Katani asihame, alipoulizwa kuhusiana na sakata hilo alisema ni kweli alizungumza na Katani kipindi ambacho tayari “nilikwishatoka Ikulu kuzungumza na Rais John Magufuli mbali na mengine nilimwambia ‘Hekima, umoja na amani inalisimamisha Taifa.”

“Taifa hili ni letu sote na Tanzania ikiharibika, sote tunaangamia,” alisema Mbatia ambaye ni mwenyekiti wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) huku akiahidi wiki hii kuzungumzia undani wa mazungumzo yake na Rais Magufuli.

Kuhusu Katani, Mbatia alisema; “Ni kweli aliniambia anataka afanye uamuzi mgumu kwa sababu anaona kuna giza nene katika chama chake (CUF).”

“Baada ya kunieleza hayo nilimweleza mambo manne ambayo ni majukumu ya mbunge tuliyofundishwa na spika mstaafu Pius Msekwa yanayopaswa kuzingatia kabla ya kufanya uamuzi.

Mbatia aliyataja mambo hayo kuwa ni taifa lake, jimbo lake, chama chake na mwisho dhamira binafsi.

“Nilimweleza kama anataka kufanya uamuzi afuate haya na haya alitufundisha Mzee Msekwa,” alisema Mbatia

Alisema mbali na Mzee Msekwa, aliyekuwa mwanasiasa kongwe nchini, Marehemu Kingunge Ngombale- Mwiru aliyewahi kusema, “Kabla ya kufanya uamuzi weka mbele maslahi ya nchi.”

Alisema hakujua kama Katani alikuwa anataka kuhama au ni uamuzi gani, “Lakini mimi nilimweleza hayo mambo manne na tukaachana.”



Chanzo: mwananchi.co.tz