Dar es Salaam. Mwanasiasa mkongwe nchini Tanzania, James Mapalala amefariki dunia katika hospitali ya Kairuki alikokuwa akipatiwa matibabu.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumatano Oktoba 23, 2019 mtoto wa mwanasiasa huyo, Bernard James amesema baba yake amefariki dunia leo saa 4:30 asubuhi.
“Alikuwa hospitali tangu wiki mbili zilizopita baada ya kusumbuliwa na maradhi ya kupumua,” amesema James.
Amesema familia imekusanyika nyumbani kwao Kinondoni kupanga ratiba ya mazishi.
Mapalala aliyezaliwa Februari Mosi, 1936 ameacha mke na watoto kadhaa.
Alikuwa miongoni mwa wanasiasa wa kwanza waliojitosa kudai mfumo wa vyama vingi urejeshwe nchini Tanzania.
Pia Soma
- RC Mbeya aruhusu wanafunzi nane wafukuzwe shule
- Baba aeleza mauaji ya mwanaye yalivyokatisha ndoto kuwa muuguzi
- KAKAKUONA: Tunasubiri Rais afoke ndiyo mambo yaende?
Kufuatia madai hayo, Mapalala alifungwa miaka miwili mkoani Lindi kuanzia mwaka 1986 hadi 1989 na baada ya kutoka aliwekwa kizuizini kwa kipindi cha mwaka mmoja katika kisiwa cha Mafia baada ya kuanzishwa chama cha siasa wakati sheria ilikuwa hairuhusu.
Alianzisha Chama cha Wananchi (CCW) mwaka 1991 na baadaye kiliungana na chama cha Zanzibar – Kamahuru na mwaka 1993 kuzaliwa Chama cha Wananchi (CUF).