Dar es Salaam. Msajili wa vyama vya siasa nchini Tanzania, Jaji Francis Mutungi amevitaka vyama vya siasa kuweka itikadi zao pembeni na badala yake vitumie ushawishi kuwaleta Watanzania pamoja ili waweze kukabiliana na ugonjwa wa virusi vya corona.
Jaji Mutungi amebainisha bila kufanya hivyo ugonjwa huo utaendelea kusambaa na athari zake zitaonekana kijamii, kisiasa na kiuchumi.
Taarifa ya Jaji Mutungi aliyoitoa jana Alhamisi Machi 19, 2020 alisema vyama vyote na wadau wa siasa wanapaswa kuunga mkono jitihada na miongozo iliyotolewa na Serikali ili kupambana na maambukizi ya ugonjwa huo ambao umeingia nchini humo.
Tayari watu sita wameripotiwa kuwa na corona huku Serikali ya Tanzania ikiwataka wananchi kuchukua tahadhari ikiwamo kuzuia mikusanyiko ya watu.
“Nitumie fursa hii kuvisihi vyama vya siasa viendelee kuwa mstari wa mbele kuhamasisha wanachama na wafuasi wenu wanatekeleza kwa vitendo maelekezo yaliyokwisha tolewa,” alisema
“Ugonjwa huu ni hatari kama wataalamu wanavyoelimisha na athari zake ni pana, hivyo kama taifa tunatakiwa kushikamana katika kukabiliana na maambukizi yake,” alisema Jaji Mutungi