RAIS John Magufuli amevitaka vyama vya siasa nchini kuepeuka matusi na vurugu katika kampeni za uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
Akizungumza katika bunge Jijini Dodoma leo kabla ya kuvunjwa kwa bunge hilo ,Rais Magufuli amesema kuwa Serikali imeshaanza maandalizi kuelekea uchaguzi huo na hivyo kuwahimiza wanasiasa wenye nia ya kuwania nafasi za uongozi kujitokeza, lakini akaonya kutumika kwa matusi na vurugu katika uchaguzi huo.
“Wapo baadhi yenu walioonyesha nia ya kuwania tena na wapo waliotangaza kutowania tena nawatakia maisha mema wale waliotangaza kustaafu na nina watakia kila la kheri wale wanaowania tena” amesema Rais Magufuli
“Nawasihi wagombea kuepuka matusi na vurugu nchi hii ya Tanzania ni yetu sisi wote, tujiepushe sana shetani wa matusi” amesema
Rais Magufuli pia ameviomba vyama vya siasa nchini kutoa kipaumbele kwa wanawake ,vijana na watu wenye ulemavu katika kuwapa nafasi za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi.
Tayari baadhi ya vyama vya siasa nchini vimeshatangaza kuanza kwa michakato ya ndani ya vyama kuchukua na kurejesha fomu kwa watia nia katika nafasi za udiwani, ubunge na urais.