Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

JPM aahidi kumpa kazi Nassari kwa uzalendo

F0cb24be32aeaa52c85ef0978f6256a1 JPM aahidi kumpa kazi Nassari kwa uzalendo

Sat, 24 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MGOMBEA urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli amesema akichaguliwa kuwa Rais, atawapa kazi wapinzani wenye kujitambua na uzalendo akiwamo aliyewahi kuwa Mbunge wa Arumeru kwa tiketi ya Chadema ambaye sasa amehamia CCM, Joshua Nassari kwa kuwa maendeleo hayana chama.

Aidha, akiwa katika mkutano wa kampeni za urais Usa River, wilayani Arumeru juzi, Magufuli alistaajabu kuona umati mkubwa wa watu waliofika kumsikiliza na kuahidi kwamba umati huo umemuachia deni la kuwatumikia wananchi wa wilaya hiyo huku akisema wapinzani wa maendeleo wataisoma namba.

Magufuli alisema: “Namshukuru sana kijana huyu Nassari, ni kijana anayejitambua, alijua alikuwa amekosea, nami nakwambia nitakupa kazi, ukafanye kazi,” Magufuli alimweleza Nassari aliyemuita jukwaani ili awaombee kura wagombea wa CCM.

Magufuli baada ya kushinda urais mwaka 2015, alimteua aliyekuwa mgombea wa urais wa chama cha ACT-Wazalendo, Anna Mghwira kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro mpaka sasa.

Pia alimteua aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu na mshauri wa Chadema na baadaye mshauri wa ACT-Wazalendo, Profesa Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji.

Akiomba kura Nassari alitumia fursa hiyo kuwaomba radhi wananchi wa Arumeru na kuwaeleza kuwa alikosea sana kwa muda mrefu kuomba kura zipelekwe upinzani katika jimbo hilo lakini sasa amefunguka macho na kuwaomba kura zote wawapigie wagombea wa CCM.

“Mtu anayeomba radhi ni jasiri, Mkuu kama kuna mahali nimewahi kukosea naomba unisamehe, niombe radhi kwa watu wa Meru mwaka 2000, nyie ni shahidi niliomba kura zipelekwe kwingine, yule leo anakuombea kura wewe mheshimiwa Rais. Turudie azimio la 1952… kumpeleka Magufuli tena Ikulu.

“Naomba ndugu zangu wa Meru kama kuna sehemu niliwakosea naomba mnisamehe. John Palangyo (mgombea ubunge wa CCM na mbunge aliyemaliza muda wake), kwa mwaka mmoja amefanya mengi. Langu leo mheshimiwa Rais Magufuli ni kukushukuru, mwaka 2014 tulizindua Chuo cha Nelson Mandela mgeni rasmi akiwa Rais mstaafu Jakaya Kikwete akachelewa mvua kidogo.

Nassari alisema alimfuata Magufuli akiwa Waziri wa Ujenzi kumueleza kuhusu hiyo barabara iliyokuwa mbovu ina gharimu Sh bilioni 1.8 na Tanroads mkoa wakatoa hela ikatengenezwa, ikawa inakosa Sh milioni 500 na alipomfuata Magufuli, alitoa hiyo hela hiyo na barabara ikatengenezwa.

“Hii ndio sababu wapinzani walipoitaka na kukubaliana kufunga midomo kwa plasta bungeni mimi sikuwahi kufunga mdomo kwa plasta bungeni. Kituo cha afya leo huduma kwa kila mtu bila kujali chama.

“Nilivyovuliwa ubunge wakadhani nimechacha, Serikali ya Uingereza ikanichukua ikanisomesha masters (uzamili) ya kwanza, amilia ya Obama wakanichukua tena na kunisomesha masters ya pili. Ndugu zangu baada ya hapo nimefunguka macho,” alisema Nassari.

“Tulipokuwa upinzani tukasema CCM imeua shirika la ndege, tanzanite pekee Tanzania, mikataba mibovu ya madini tulipiga kelee, mzee huyu amerekebisha sheria za madini, nani asiyejua leo tanzanite ipo Tanzania pekee? Shirika la ndege limerejea, ukija hapa jisikie nyumbani, hapa ni nyumbani kwako mzee,” alisema Nassari.

Magufuli huku akishangazwa na umati wa watu Usa River, alisema, “Nataka niseme kwa hali hii wataisoma namba, nataka niahidi, umati huu umeniachia deni kubwa la kuwafanyia kazi Arumeru, nataka nikiri mbele yenu sintawaangusha kamwe.

“Kama hapa Usa River watu wanakuwa wengi kuliko mikoani wananifanya nifikirie mambo mengi sana. Tumuachie Mungu ngoja tumalize uchaguzi ntajua nini cha kufanya,” alisema Magufuli huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu waliofika kumsikiliza.

Chanzo: habarileo.co.tz