Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Heche atumia ahadi za uchaguzi za CCM kuchangia bajeti 2019/20

63495 Hechepic

Wed, 19 Jun 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dodoma. Mbunge wa Tarime Vijijini (Chadema) John Heche ametaka Waziri wa Fedha na Mpango  Dk Philip Mpango kueleza ni vipi wametekeleza ahadi sita walizozitoa katika uchaguzi mkuu 2015 ikiwemo kutoa Sh50 milioni kwa kila kijiji.

Akichangia mapendekezo ya bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 ya Sh33.1 trilioni,  leo Jumatano Juni 19, 2019, Heche amesema hii ni bajeti ya nne ya awamu ya tano.

Amesema bajeti ya  mwakani itakuwa sio ya kwao kwa sababu Serikali itakayokuja kutekeleza ni ya awamu ya sita ambayo CCM kwa imani yake watakuwa wametoka madarakani.

“Tuko hapa kwa ajili ya kuwakumbushia ahadi mlizoahidi wakati wa uchaguzi, mojawapo ya ahadi ni kuwa mtapeleka milioni 50 iko wapi hiyo Sh50?”amehoji.

Ahadi nyingine aliyoizungumzia ni pesheni kwa  wazee ambayo bado haijatekelezwa na kutaka waizungumzie maana waliitaja katika ilani ya uchaguzi.

“Hampaswi kuchaguliwa hata kijiji kimoja kwasababu hamstahili. Mliahidi pia kuongeza ajira,”amesema.

Pia Soma

Amesema kati ya mwaka 2010 hadi 2014 serikali ya awamu ya nne iliajiri watumishi wa sekta ya afya  42,800 lakini awamu ya tano wameajiri watumishi 10,000 pekee.

“Tunaenda mbele nyuma mnapaswa kuchaguliwa ama la. Mmepunguza ajira ya zaidi ya 30,000,”amesema.

Amesema wazazi wamejikamua na kuwasomesha watoto wao katika vyuo mbalimbali vya ualimu nchini.

Heche amesema tangu mwaka 2015 wanafunzi waliomaliza katika vyuo mbalimbali vya ualimu walikuwa ni 75,000 na kuhoji ni wangapi walioajiriwa.

“Unatembelea VX na sisi tunalipwa fedha. Tueleze mnapaswa kuchaguliwa. Mnawaacha mtaani mnawaambia waendelee kula mtori nyama ziko chini. Tunataka majibu ni fedha za walipa kodi utuambie unatoa lini ajira,”amesema.

Heche amesema pia wameahidi kuwa wataongeza mishahara na kupunguza kodi katika mishahara (PAYE) lakini hawajatekeleza ahadi hiyo.

Pia Heche amemtaka Dk Mpango amjibu kuwa mradi wa kufua umeme wa maji wa Stiglers Gorge ambao amesema utatumia Sh7 trilioni hadi kukamilika utatumia miaka mingapi kuzalisha megawati 2100.

Chanzo: mwananchi.co.tz