Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Hatutatoka nje ya reli kwenye kampeni-CCM

4fbaa49589fef871606e3f5d3549c902 Hatutatoka nje ya reli kwenye kampeni-CCM

Sun, 18 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kimefanya kampeni za kistaarabu na kitaendelea kufanya hivyo bila kutoka nje ya reli kutokana na vitendo visivyokubalika ambavyo vimekuwa vikifanywa na baadhi ya wagombea wa vyama vingine.

Aidha, chama hicho kimeeleza ratiba ya kampeni zake za ‘lala salama’ ambazo kesho, mgombea urais wake, Rais John Magufuli atakuwa mkoani Pwani na baadaye mikoa ya kaskazini kabla ya kurejea Dodoma tayari kwa kupiga kura Oktoba 28.

Hayo yalisemwa na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole wakati akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam jana. “CCM tumefanya kampeni ya kistaarabu.

Lakini mnafahamu kwamba kumekuwa na kauli za kichochezi,” alisema na kutaja mgombea wa urais visiwani Zanzibar aliyezungumza hadharani akiwataka wafuasi wake wachukue mapanga, mundu na mawe wawe tayari.

Alisema yupo mgombea mwingine ambaye amekuwa akihimiza wafuasi kujiandaa kwa maandamano baada ya uchaguzi. “CCM inahimiza wakishapiga warudi nyumbani ushindi unakuja,” alisema.

Alisisitiza, “Tumejipanga kufanya kampeni za kistaarabu… hatutatoka nje ya reli. Kumekuwa na vitendo visivyokubalika kutoka kwa upinzani na kinyume cha sheria, katiba ya nchi na kinyume na taratibu tulizojiwekea na maadili ya uchaguzi.”

Alisema vitendo visivyokubalika vinavyoendelea kufanywa na wagombea wa vyama vya upinzani kuwa vinatokana na kukosa sera hivyo wanafanya makosa ili wakiadhibiwa walalamike kuwa uchaguzi haukuwa huru na wa haki.

Alitaka umma wa Watanzania kupuuza na tuwafundisha watu hao kwamba Tanzania imejipanga kupiga maendeleo makubwa na kutambua kwamba amani ni tunu yao, umoja na mshikamno havitafanyiwa mchezo.

Polepole alisisitiza kuwa amani ni jambo la msingi katika taifa na kuwahakikishia wananchi kuwa CCM inaendelea kusimamia serikali kuhakikisha amani inakuwa madhubuti wakati wote.

Alisema mafanikio ya nchi yaliyopatikana kwa muda mfupi, yametengeneza maadui wengi na kwamba kipindi ambacho wamesimama imara na madhubuti ni kipindi hiki cha uchaguzi.

“Asiwatishe mtu, asiwaogopeshe mtu.” “Ninawaomba wana CCM wote , waendelee kulinda amani, sisi hatutaki kwaruhusu vijana wetu kufanya vurugu, hata baada ya kupiga kura tunawashauri wakatulie nyumbani kam sheria zinavyosema,” alisema Polepole.

Ratiba ya kampeni Polepole alisema Magufuli ataendelea na kampeni mkoani Pwani na baadaye Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Manyara na kisha Dodoma.

Mgombea mwenza, Samia Suluhu Hassan ambaye jana alikuwa Dar es Salaam kwa kazi za kiserikali, atakwenda Zanzibar na kufanya mikutano Unguja na Pemba na kisha atakwenda Morogoro. Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, atakwenda Mtwara na Lindi.

Chanzo: habarileo.co.tz