Dar es salaam. Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Halima Mdee amerudisha fomu ya kuwania nafasi hiyo katika uchaguzi utakaofanyika kuanzia Desemba 10, 2019.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumamosi Novemba 30, 2019, Mdee amesema alichukuliwa fomu na wanawake wa baraza hilo na kumuomba agombee tena, aliijaza na kuirudisha jana.
"Jana nimerudisha fomu sasa nasubiri vikao vya uteuzi ili nianze kampeni,” amesema Mdee.
Mbunge huyo wa Kawe amewataka wanawake kuacha woga, akiwataka wajitokeze kuchukua fomu kuwania nafasi mbalimbali za uongozi.
Katibu wa Bawacha, Grace Tendega amesema waliochukua fomu ni ngumu kuwafahamu, watakaporejesha ndipo watajulikana.
"Siwezi kuwa na idadi ya watu waliochukua fomu kwa kuwa fomu zinachukuliwa maeneo mbalimbali ikiwemo mikoani kwenye ofisi za Kanda, tusubiri zoezi litakapohitimishwa tutakuwa na idadi kamili," amesema Tendega.