Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Gwajima, Tarimba watamba kushinda kwa kishindo

872af9374f255557d6c3e54e86e7aaf5 Gwajima, Tarimba watamba kushinda kwa kishindo

Mon, 26 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

UTAFITI uliofanywa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Kinondoni imebainisha kuwa wagombea wa chama hicho kwa nafasi ya ubunge katika majimbo ya Kinondoni na Kawe watashinda kwa kishindo kura zitakazopigwa keshokutwa.

Kwa mujibu wa chama hicho mgombea ubunge jimbo la Kawe Askofu Josephat Gwajima atashinda kwa asilimia 80 hadi 84 na pia mgombea jimbo la Kinondoni Abbas Tarimba atashinda kwa asilimia 90.

Aidha, utafiti huo umeonesha kuwa katika majimbo hayo mgombea urais kwa tiketi ya CCM John Magufuli atazoa kura zaidi ya asilimia 93 katika majimbo yote mawili.

Mameneja wa kampeni wa majimbo hayo ambao ni Benjamin Sitta (Kawe) na Mohammed Mtulia (Kinondoni) waliyasema hayo jana wakati wakizungumza na waandishi wa habari kuhusu tathmini hiyo.

Sitta alisema, tathmini hiyo imetokana na namna Gwajima alivyowafikia wakazi wa jimbo hilo kupitia kampeni alizofanya. Alisema tangu aanze kampeni amekuwa akitumia mbinu kuwafikia wananchi ikiwemo kwenda nyumba kwa nyumba, mtaa kwa mtaa, na kijiwe kwa kijiwe.

Kwa mujibu wa Sitta mgombea huyo aliwafikia watu zaidi ya 150,000 na alifanya mikutano ya hadhara iliyowafikia watu zaidi ya 370,000.

“Mgombea wetu ametembea kwa miguu kwenye barabara, maji na lami zaidi ya kilometa 400 na huko kote alifanikiwa kugundua kero na migogoro inayowasumbua wananchi wa Kawe na baadhi ya kero alizitatua kabla hata ya kupata ridhaa ya kuwa mbunge wa wananchi wa jimbo hilo,” alisema.

Sitta alimshukuru Rais Magufuli kwa kuitikia wito wa mgombea huyo na kuwatembelea wananchi wa Basiaya Boko waliokumbwa na mafuriko hivi karibuni na kufanikisha kupatiwa kiasi cha Sh bilioni tano za kuwasaidia.

Alisema kipindi chote cha kampeni, Chama hicho kilikuwa na timu ya watu waliokuwa wakifanya tathmini ya uwezo wa mgombea huyo ambayo ilitumia mbinu mbalimbali ikiwemo kuwahoji wananchi, kuwapigia simu na kuwatumia wajumbe wa nyumba10 kukusanya maoni.

“Tathmini ilionesha wazi kuwa Askofu Gwajima ana mvuto wa pekee Kawe, yeye pekee ana waumini zaidi ya 70,000 wakati Kawe ina jumla ya wapigakura 412,000.

Timu hiyo ilihoji watu 1, 000 hadi 5, 000. Kati ya watu 1, 000, watu 970 walisema wanamchagua Gwajima, 20 wanachagua upinzani,” alisema.

Aidha, alisema kati ya watu 5,000 waliohojiwa4,705 walisema wanamchangua Gwajima, 100 upinzani na 50 wako katikati.

“Kwa tathmini hii tunaimani kuwa CCM safari hii Kawe itapata kura wastani wa 324,000 sawa na asilimia 80 hadi 85”alisema Sitta.

Mtulia alisema kwa mujibu wa ripoti ya utafiti ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu jimboni humo, Tarimba ana uhakika wa ushindi wa asilimia 90 na Magufuli akipata ushindi wa asilimia 93.

Alisema ushindi huo unatokana na ubora wa Tarimba ambaye ni kada wa siku nyingi anayekubalika katika jimbo hilo. “Mimi niligombea jimbo hili kutetea nafasi yangu, lakini Kamati Kuu iliona ubora wa Tarimba hata mimi simfikii na ninaiunga mkono,”alisema Mtulia.

Alitaja sababu nyingine ya ushindi huo kuwa ni CCM kuingia kwenye uchaguzi mwaka huu, huku wanachama wake wakiwa wamoja bila makundi lakini pia kazi kubwa iliyofanywa na Magufuli katika kipindi chake cha kwanza cha urais katika masuala ya maendeleo.

Alisema, pia mgombea huyo amefanya kampeni kabambe kwa mtindo wa nyumba kwa nyumba, wajumbe wa nyumba 10 na mikutano ya hadhara.

“Kinondoni ni jimbo lenye wapigakura 370, 000 CCM tuna wanachama 67,000 na ili ushinde unahitaji kura kama 150,000 hivyo tulihitaji kutafuta kura 100,000 za wasiokuwa wanachama wa CCM na kupitia kampeni zetu tumewafikia wanachama zaidi ya 180,000,” alisema.

Pamoja na hayo, alieleza kuwa ushindi Tarimba pia utatokana na udhaifu wa wagombea kutoka upinzani ambao katika majukwaa kwa sasa badala ya kutoa hoja na ahadi zao kwa wananchi wanatoa tuhuma na matusi dhidi ya wagombea wenzao.

Askofu Gwajima alikanusha tuhuma dhidi yake ikiwemo zinazomhusisha kutoa ahadi za uongo na kueleza kuwa pindi atakapopatiwa ridhaa ya kuliongoza jimbo la Kawe, wananchi watashuhudia uwezo wake.

Alisema ana mipango mingi akishirikiana na washirika wake ikiwemo kutumia malighafi ya Kawe kuwa na ukanda wa bahari kwa kununua boti ndogo zitakazotoa ajira kwa vijana.

Chanzo: habarileo.co.tz