MBUNGE wa Viti Maalum (Chadema), Grace Tendega amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC).
Tendega ambaye amefukuzwa uanachama wa chama hicho, kufuatia kupatikana na tuhuma za usaliti, amechaguliwa kushika nafasi hiyo leo Jumatatu mjini Dodoma.
Nafasi ya makamu mwenyekiti wa LAAC, imechukuliwa na Suleiman Zedi (CCM).
Wabunge hao wawili, walikuwa wagombea pekee kwenye nafasi hizo na kila mmoja amepata kura 22. Kamati hiyo, ina jumla ya wajumbe 25.
Tendega, pamoja na wabunge wengine 18 wa Viti Maalum ambao walikuwa wanachama wa Chadema, walifutwa uanachama wa chama hicho na Kamati Kuu (CC), iliyokutana Novemba mwaka jana.
Wote kwa pamoja, walituhumiwa kwa usaliti ndani ya Chadema, kujipeleka bungeni kuapishwa bila idhini ya chama hicho, udanganyifu, ugombanishi, kuchochea migogoro na kushirikiana na wanaokitakia mabaya chama hicho kikuu cha upinzani nchini.