Mbeya. Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kupitia taasisi yake ya Tulia Trust ametumia Sh820.39 milioni kutekeleza shughuli mbalimbali za kijamii jimbo la Mbeya Mjini linaloongozwa na mbunge wa Chadema Joseph Mbilnyi au Sugu.
Dk Tulia ametumia fedha hizo kwa miaka mitatu ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Mbali na hilo, Dk Tulia ametumia Sh93.67 milioni kuchangia ujenzi na kuimarisha CCM Mbeya Mjini na mkoa wa Mbeya.
Hayo aliyasema juzi akiwasilisha na kukabidhi taarifa yake ya utekelezaji Ilani ya CCM na shughuli alizofanya kuanzia 2015 katika kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Mbeya Mjini.
Dk Tulia alisema Sh820.39 milioni alisaidia sekta za elimu, afya, maji, miundombinu, uwezeshaji mikopo kwa vikundi na utawala zilizotolewa na taasisi yake ya Tulia Trust na kutoka mfukoni mwake zilitumika Sh93.67 milion.
Alisema ataendelea kutekeleza Ilani ya CCM kwa vitendo huku akiomba zaidi ushirikiano wa dhati kutoka kwa wananchi, chama na viongozi wa ngazi zote.
Awali, mwenyekiti wa CCM Mbeya Mjini Hamphrey Msomba, alisema CCM inapaswa kujipanga ili kushinda uchaguzi ujao wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu, huku akitaja sababu saba kushinda. Miongoni mwa sababu hizo ni kusimamia na kutekeleza ahadi katika jimbo la Mbeya Mjini.