Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa chama tawala nchini Tanzania cha (CCM) Dk Bashiru Ally amewataka wanachama wa chama hicho kuzingatia majina yenye ujumbe kwenye mashina wanayofungua badala ya kutaja majina ya wagombea.
Dk Bashiru ameyasema hayo leo Jumapili Septemba 1, 2019 wakati akizindua shina la ‘hapa kazi tu’ kata ya Kawe wakati wa ziara ya uimarishwaji wa chama hicho jijini Dar es Salaam nchini Tanzania.
Amesema majina yanayotakiwa ni yale yanayobeba ujumbe wa chama na Serikali na siyo majina ya wagombea katika nafasi mbalimbali.
"Tunataka majina yanayobeba ujumbe wa chama na Serikali na sio majina ya wagombea kwa kuwa chama hiki kina historia katika nchi hii," amesema Dk Bashiru
Amesema hakuna atakaye nyanyaswa na kero mbalimbali zinazowakabili zitashughulikiwa na Meya wa Kinondoni, Benjamin Sitta na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo ambao ameambatana nao kwenye ziara hiyo watazishughulikia.
"Hakuna atakayenyanyaswa, mkiona mnasumbuliwa pigeni simu kwa mkuu wa wilaya, mkuu wa mkoa na wasipowasikiliza nipigieni mimi," amesema