Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa chama tawala nchini Tanzania (CCM), Dk Bashiru Ally amesema hatoshangaa wabunge wa chama chake kupitwa bila kupingwa wakati wa mchakato wa ndani wa kuwachagua wagombea watakaopeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao 2020.
Dk Bashiru ameyasema hayo leo Jumanne Julai 30, 2019 wilayani Ilemelea mkoani Mwanza wakati akizungumza katika mkutano wa kuangalia utekelezaji wa Ilani ya CCM jimbo la Ilemela linaloongozwa na Angelina Mabula ambaye pia ni Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara, Dk Bashiru ambaye pia ni mlezi wa mkoa wa Mwanza amesema hategemei wakazi wa Ilemela kufanya kosa kwa kuwa mbunge wao Angelina Mabula anafanya kazi nzuri.
“Sitashangaa kama akipita bila kupingwa, sitashangaa kwa wabunge wengi na madiwani wengi kupita bila kupingwa. Na sio kwamba nampigia kampeni hapana yeyote na aje ila ajue kwamba kiti kimekaliwa na aliyekalia ameenea. Ole wake mtu anayetaka mlango wa nyuma, hatutaki fujo kwenye chama chetu tunataka utulivu.”
“Wapo watakaosema tunaua demokrasia ndani ya chama, demokrasia ni maridhiano tukishakubaliana ndani ya chama, wewe endelea na mambo yako kwenye chama chako,” amesema Dk Bashiru
Katibu Mkuu huyo pia amesisitiza kwamba chama hakitawabeba viongozi walioshindwa kutimiza majukumu yao na kukiangusha chama.
Pia Soma
- Serikali yatumia mawakili 10 kupinga hukumu ya Ma DED
- Mahakama Kenya yamzuia gavana Waititu kuingia ofisini
- Kilichojiri kesi anayedaiwa kumuua mkewe, kumchoma moto hiki hapa