Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Richard Kasesela amesema kuwa anamtakia kila la kheri Mchungaji Peter Msigwa ambaye ametangaza nia ya kuwania kiti cha Urais kupitia CHADEMA kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Akizungumza na kituo cha runinga mtandao cha Habari Kwanza, Mkuu huyo wa Wilaya ya Iringa Mjini amesema ‘’nimesikia ametangaza kugombea Urais, nimtakie kila la kheri na nimpe pongezi kwa yeye kukimbia jimbo na kwenda kugombea urais, lakini najua tu atarudi jimboni. Kule kwenye Urais hawezi kupata kwa taratibu zao ninavyozijua’’.
Alipoulizwa kwanini anafikiri kuwa hawezi kupata nafasi ya Urais, Mkuu huyo wa wilaya amedai kuwa (CHADEMA) wana watu wao wamewapanga na hii ni mpango tu kuonesha kuwa wanagombea Urais.
‘’Wana watu wao wamewapanga na hii ni gagari tu wanatuonesha sisi anataka kugombea urais. Lakini cha pili, kama ameshindwa kuongoza wilaya, ataweza Urais? Tunachojua sisi hapa amekwama na ameshindwa kuongoza wilaya. Kwahiyo kwenue Urais, sidhani kama atafanikiwa’’, amesema Bw. Kasesela
Hivi karibuni, Mchungaji Peter Msigwa ambaye ni Mbunge wa Iringa Mjini kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo alitangaza kuwa amewasilisha kwa katibu Mkuu wa Chama hicho barua yenye nia ya kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
Ikiwa atapitishwa na chama hicho, anatarajiwa kukabiliana na upinzani mkali kutoka kwa anayetarajiwa kuwa mgombea kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Dkt. John Pombe Magufuli na vyama vingine vya Upinzani kama CUF na NCCR Mageuzi.