Katibu mkuu wa CCM, Daniel Chongolo ameahidi kuwaondoa kwenye nafasi zao watendaji wa jumuiya za wazazi wasiofanya kazi za ulinzi wa watoto.
Chongolo amesema kutakuwa hakuna haja ya kuwa na viongozi wa jumuiya hiyo ambao hawafanyi kazi kwenye jamii zao ambako matukio mengi ya kikatili yanatokea.
Chongolo ameyasema hayo leo Alhamisi Juni 16, 2022 wakati akifungua mkutano mkuu wa baraza la jumuiya ya wazazi Taifa jijini Dodoma.
“Sasa hivi matukio ni mengi ya ukatili kwa watoto lakini kuna baadhi ya watu wana vyeo vikubwa hawafanyi chochote, lazima kwa uaminifu mliopewa kama wazazi mwajibike."
"Mnatakiwa msimame kama jumuiya ya wazazi, nendeni mkemee matendo hayo, matendo yenu yaendane na nafasi zenu. La sivyo tuue hayo majina makubwa yasiyo akisi dhana za nafasi mlizopewa,"amesema.